Ticker

10/recent/ticker-posts

Angalia hii kauli ya What Would Magufuli Do inavyoanza kuwatesa Wakenya live

   

Na Mwandishi Wetu, Addis Ababa

Bomba la Mafuta:
WIKI hii nchi tatu za Afrika Mashariki zipo katika kile kinachoweza kufananishwa na sintofahamu kuhusu ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Uganda hadi Pwani ya Afrika Mashariki. Mradi huo mkubwa unalenga kuisaidia Uganda kulifikia soko la kimataifa.
Takwimu zinaonesha kuwa Uganda ina kiasi cha hazina ya mafuta inayofikia mapipa bilioni 2 (na utafutaji unaendelea) kiasi ambacho Serikali ya nchi hiyo inapanga kukisafirisha kama mafuta ghafi kwnda nje ya Afrika na sehemu nyingine kusafishwa ndani ya Uganda na pia katika soko jirani la Rwanda, Kenya na Tanzania.
Kufikia hali ilivyo sasa kuna mengi yametokea ambapo Kenya ndiyo ilikuwa ya kwanza “kuanza mazungumzo” na Uganda juu ya ujenzi wa bomba hilo kwa njia ya Kaskazini. Mazungumzo haya kwa tathmini yangu yalikwama kwa sababu Kenya walileta mazoea na pia kuegama zaidi katika “biashara” kuliko “ubia” wenye maslahi mapana ya kikanda.
Katika makala haya nitajaribu kujenga hoja kwa nini mradi huo sasa umeangukia mikono salama ya Tanzania baada ya siasa na sanaa za muda mrefu za Kenya katika mradi huu muhimu kwa ukandi wetu wa Afrika Mashariki. Zipo sababu nyingi lakini hapa nitajadili mambo matatu: usalama, gharama za mradi na pia mabadiliko ya kisiasa katika ukanda huu kufuatia ujuo wa Dkt John Pombe Magufuli wa Tanzania.
 Usalama
Ukweli wa muhimu katika uamuzi kuhusu mradi huu ni usalama. Nairobi inapaswa kujua na kuwa na huruma kwa wananchi wake, Waganda na raia wengine wa Afrika Mashariki kwa sababu kuupeleka mradi huu njia ya Kaskazini kutoka Bandari ya Lamu ni sawa na kuwapa Al-Shaabab kisu na kuku wajichinjie wenyewe kitoweo cha mchana.
Huu ni ukweli wenye uhalisia na sio propaganda kama Kenya wanavyotaka kujaribu kuwapumbaza wananchi wa Afrika Mashariki kuhusu mradi huu. Tafiti nyingi zimefanyika na kuchapishwa kuonesha kuwa njia hiyo ya Kaskazini ni hatari kiusalama tena katika Kenya ambayo mara kadhaa imeshindwa hata kuwalinda raia wake wenyewe.
Ni bahati nzuri pia kwamba kampuni ya Total iliyo tayari kutoa kiasi cha dola za Marekani  bilioni 4 kuufadhili ujenzi huo kwa njia ya Kusini (kuanzia Bandari ya Tanga) nayo inaguswa sana na suala hili la usalama.
Total sio watu wa kuambia kuhusu ubaya wa usalama dhaifu katika sekta ya mafuta na gesi na wala sio watu wa kuhakikishia usalama kupitia makaratasi na “power point presentations” kama wanavyofanya Kenya.
Kampuni hiyo inayosimamia sehemu kubwa ya mafuta ya Uganda imepata kukumbana na matukio mengi kwingineko duniani ya wafanyakazi wake kushambuliwa na hata kuuawa wakiwa katika ujenzi au usimamizi wa miradi kama hiyo.
Mwaka huu wafanyakazi 11 wa Total waliuawa katika moja ya visima vya mafuta wanavyovisimamia nchini Libya katika shambulio linaloaminika kutekelezwa na wafuasi wa kundi linaloungwa mkono na Islamic State.
Kampuni hiyo pia ina uzoefu mwingine kwa kuwa inamiliki visima katika eneo lililo katikati ya vita la Yemen na Algeria ambako mwaka 2013 wapiganaji wanaoaminika kuwa wenye uhusiano na Al-Qaeda waliwaua wafanyakazi 40 waliokuwa wakiwashikilia mateka katika kisima kimoja cha gesi
Kwa uzoefu huu wa Total lakini pia kwa manufaa ya Uganda na ukanda mzima wa Afrika Mashariki, Nairobi inapaswa kukubali kuwa ingawa mradi huu kwao ulikuwa na malengo mengi na ya kibiashara kwao lakini Uganda na EAC hatupaswi kujiingiza katika hatari iliyo wazi ya kiusalama.
Ripoti moja ya taasisi ya Practical Action inaonesha eneo la Kaskazini mwa Kenya lilivyosheheni usafirishaji haramu wa silaha, somo kutoka shambulizi dhidi ya Chuo Kikuu cha Garissa na ukweli kwamba sehemu ya bomba itapita ukanda mrefu usio na makazi ya wala wa vijiji vya karibu, vyote vinaashiria urahisi kwa Al-Shaabab.

Katika hili, Rais Kenyatta anapaswa kuwa muungwana tu kuruhusu mradi huo uendelee kwa njia ya Tanzania huku yeye akiangalia zaidi biashara na Sudani Kusini au kama walivyopendekeza Wakenya wengi katika mtandao wa gazeti la The Daily Nation wengi wameshauri “Serikali ya Kenya iangalie zaidi namna ya kusafirisha hazina ya mafuta waliyo nayo.”   
                                    Gharama za Mradi
Jambo la pili ambalo harakati za Kenya zinashangaza ni ukweli huu wa, ukiacha lile la gharama ya usalama, lakini pia ukweli kwamba kwa jiografia ya njia ya Kaskazini, mradi huu utakuwa na gharama kubwa.
Hali hiyo inaweza kuwa na madhara makubwa kwa uchumi wa Uganda na majirani zake kwani mafuta ya nchi hiyo yatakuwa ya gharama kubwa zaidi ya inavyotarajiwa. Takwimu za wataalamu zinaonesha kuwa kwa njia ya Kaskazini itakayoanzia katika Bandari “ambayo haipo” ya Lamu, mradi wa bomba hilo utakuwa wa gharama kubwa kwa namna nne.
Mosi, ujenzi wa mradi kwa njia ya bandari ya Lamu utakuwa ni takribani kilometa 1,300 lakini kwa sababu nyingine pia nitakazozieleza hapa punde ujenzi wake utapanda hadi kufikia dola za Marekani bilioni 4.5. Huu ni mzigo usio na sababu.
Kwa njia ya Bandari ya Tanga ambayo urefu wake utakuwa takribani kilometa 1,400 ujenzi wake unaelezwa utakuwa ni dola za Marekani bilioni 4.0 tu. Hii ni nafuu kwa kiwango cha trilioni moja na ushee lakini pia bado kuna gaharama nyingi nyingine pia zitapungua.
Tatu, wataalamu wa sekta ya mafuta wanasema kwa aina ya mafuta ya Uganda ambayo ni mazito hali ya hewa ya Ukanda wa Juu wa Kaskazini mwa Kenya itasababisha mafuta hayo kuganda na hivyo kuhitajika gharama zaidi za kulipasha moto mara kwa mara bomba hilo.
“Ujenzi wa mradi huu unahitaji teknolojia tofauti kidogo kama utachukua njia ya Kenya. Kwa aina ya mafuta mazito yaliyogundulika Uganda ambayo ni kama nta hivi hali ya baridi katika maeneo walikopanga lipite bomba itasababisha gharama zaidi ya kulipasha moto bomba mara kadhaa ili mafuta yaweze kusukumwa,” anasema mtaalamu mmoja aliyesimamia miradi mingi ya ujenzi wa mabomba ya gesi na mafuta Ulaya na Afrika. 
Nne, gharama nyingine ambayo wataalamu wa Kenya wanataka kuzificha ni uasili wa Bandari ya Lamu ambayo haipo kwa sasa (ndio inajengwa). Bandari hii sio ya kama ile ya Tanga hivyo inachangamoto zake katika meli kupakia na kupakua mafuta.
Mtaalamu mmoja anasema wakati Bandari ya Tanga ni ya asili na iliyozungukwa na visiwa vya karibu vinavyopunguza mawimbi na hivyo kuzipa meli urahisi wa kupakia au kupakua, kwa Bandari “inayolazimishwa” ya Lamu Serikali ya Uganda itaingia tena gharama nyingine ya kulazimika kujenga matenki mengi ya kuhifadhi kwanza mafuta hayo nje ya Bandari.
Naironi inapaswa kufahamu kuwa mradi huu ni limbuko la kiuchumi kwa Waganda na kama gharama hizi zisizo na tija zitakwamisha wananchi wa Uganda kunufaika na mafuta, Kenya itakuwa imefanya jinai ya kihistoria.   
                                                    Dkt JPM
Kitu kimoja kilicho dhahiri sasa ukiacha suala la usalama na gharama ni kwamba siasa na uchumi wa Afrika Mashariki kwa sasa zimepata msukumu mpya: ujio wa mtu huyu, Dkt. John Pombe Magufuli, kiongozi anayeamini katika sayansi badala ya siasa katika maendeleo.
Huyu ndiye kiungo mpya katika suala hili ambalo limeshalipotezea muda mrefu Taifa la Uganda na Afrika Mashariki kwa ujumla na kuzuia kufaidika na raslimali hiyo iliyopo jirani. Hii ni kwa sababu ukifuatilia mazungumzo ya njia ya Kenya yalivyochukua muda mrefu, mtu hawezi kukosea kushukuru ujio wa JPM.
Akitumia staili yake ya utambuzi wa haraka, nia njema na kutaka mambo yaende, imemchukua kikao kimoja tu na Rais mwenzake Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda na kisha kikao kimoja tu na Rais wa Total, Afrika Mashariki kwa Rais Magufuli kufanya uamuzi kuwa Tanzania itakuwa mwenyewe wa ujenzi wa bomba hilo.
Fundisho kwa Kenya ambao sasa wanaanza upya kuleta siasa za kuhaha kujaribu kuurejesha mradi huo katika njia ya Kaskazini mwa Kenya ni kwamba siasa za ukanda huu zimebadilika sana na ama wanapaswa wao nao kubadilika au kubaki wakiyatazama mabadiliko yakitokea.
Mafuta ya Afrika Mashariki yawe Uganda, Kenya au Tanzania au kwingineo kwa namna moja hayapaswi kuingiziwa siasa zitakazokwamisha wananchi wa kawaida kufaidika na raslimali hizo.
Nafahamu kwamba hakuna kitu kingine muhimu katika ujenzi huo kama muda na hili ndilo limewaliza Waganda kwa kipindi kirefu. Mradi huu ulipaswa kuwa umeanza jana kuliko kubakia katika “power point presentation” za Wakenya.
Katika mazingira kama haya na hali ilivyokuwa inakwenda kwa kusuasua nimefurahishwa na uamuzi wa Rais Museveni wa kujiuliza WhatWouldMagufuliDo?Jibu la swali hili limekuwa na kuibukia kwa mradi huo nchini Tanzania na naamini utaanza na kukamilika haraka.
Ushauri kwa Nairobi, na kama walivyosema wananchi wengi wa Kenya katika mtandao wa Daily Nation, huu sio wakati tena wa kuendekeza siasa bali watumie muda huu kuimarisha usalama kwanza katika eneo lake la Pwani na Kaskazini kasha ikamilishe ujenzi wa Bandari ya Lamu kwanza.
Kwa leo alamsiki.