Ticker

10/recent/ticker-posts

JAJI WARIOBA: KIONGOZI TANZANIA AKIWA KARIBU NA MATAJIRI WAKUBWA NI KICHOCHEO CHA RUSHWA NA ABUSE OF POWER..MFANO KAMA HUYU

Mzee Warioba akiwa ndani ya Star TV katika kipindi maalum cha Ajenda 2015.

Mtangazaji Yusuf Kamote: Una maoni gani kuhusu Mchakato wa kupata wagombea ndani ya vyama?

Jaji Warioba: Wakati tunafanya midahalo kuhusu Katiba Mpya, tuliwahi kuvionya vyama vya siasa kuhusu kuteuwa wagombea ambao wana mapungufu makubwa kimaadili. Kuna baadhi ya watu au vyama vilitubeza lakini hatukunyamaza kwa sababu taifa ni zaidi ya uanachama wa vyama vya siasa.

Jaji Warioba: Kiongozi katika Tanzania au nchi za Afrika akiwa karibu na matajiri wakubwa, hiki ni kichocheo cha rushwa na abuse of power. Niliwahi kuwa Mwenyekiti wa tume iliyochunguza masuala ya rushwa na tuligundua rushwa kubwa zinatokana na viongozi kuwa karibu sana na matajiri wakubwa.

Jaji Warioba: Tanzania kwa sasa ina tatizo la kimaadili hasa kwa viongozi wengi. Kelele zetu ziliwafanya CCM kutusikia na kuchagua mgombea ambaye anakidhi vigezo vya Rais ambaye anapaswa kujua matatizo ya Watanzania, awe mzalendo, mwadilifu, Mchapakazi na anapaswa pia kujua atafanya nini ili kuboresha maisha ya wananchi kupitia sekta za afya na uchumi.

Yusuf Kamote: Ni kweli uliombwa uwe Mgombea Urais kwa tiketi ya chama chochote?

Jaji Warioba: Ni kweli niliombwa niwe mgombea wa Urais lakini nilikataa kwa sababu nimeishaachana na front politics.

Kuna viongozi wakuu wa vyama ambao walinifuata kuniomba niwe mgombea, niliwakatalia.

Nimekuwa mwanachama kwa zaidi ya miaka 50 nimeamini sera za CCM, siwezi kesho kuamka na kusema kwa sasa siamini sera za CCM na kifanya hivyo nitakuwa ninawadanganya wananchi.

Hii dhana ya kupata wagombea kutoka chama kingine inaleta matatizo makubwa kwenye vyama vya siasa. Chama hakiwezi kukasimu nafasi ya kugombea Urais. Kama kuna chama kinaamini hivyo lazima kijiandae pia hata madaraka kukasimiwa kwa chama kingine.

Mamluki wanaweza kuharibu chama. Kwa mfano NCCR-Mageuzi kilipata matatizo makubwa baada ya kukaribisha watu kutoka chama kingine ili awe mgombea Urais pamoja na kwamba kilikuwa kimejijenga sana.

Kuna viongozi waliniomba nisiwe na upande kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu lakini niliwambia mimi ni mwanaCCM na siwezi kukaa kimya na kufanya hivyo ni kuminya uhuru wangu wa kutoa maoni na haki hata kama CCM wanafanya mambo ambayo hayana maslahi ya kitaifa.

Wakati wa ujana wetu ndani ya CCM, hatukufundishwa kuwa wanafiki na unafiki ni sumu katika taifa letu. Kuna watu na hasa baadhi ya wanaCCM hawakuelewa wakati nilipokuwa ninainyoshea kidole kuhusu mchakato wa Katiba Mpya.

Jaji Warioba: Kuna wengine walidiriki kuniuliza kwa nini sitoki CCM pamoja na kuwepo kwa baadhi ya wanaCCM waliokuwa wanasema inafaa nitoke.

Niliwaambia mimi ni CCM imani na siyo CCM Maslahi. CCM imani hawatoki kwenye chama walichojiunga kwa sababu ya sera zake.

Kuna baadhi hawakuelewa utaratibu wa chama chetu. CCM tuko tayari kuambiana ukweli pale unapoona kuna matatizo fulani ndani ya chama lakini hii haina maana kuwa hukubaliani na sera za chama.

Yusuf Kamote: Wahenga wanasema tungo huzaa neno na neno la leo huzaa dhana ya kesho au ndilo umbo la kesho. Kauli hii inasemwa na kurudiwa katika mikutano ya Kampeni kuwa tokea uhuru hakuna chochote kilichofanyika. Unaichukuaje kauli hii hasa ikizingatiwa umekuwa mwanachama tokea 1963.

Jaji Warioba: Nadhani kuna watu hawafahamu historia ya Taifa letu na kama wanafahamu basi watakuwa wanapotosha kwa faida yao wanayoifahamu wenyewe.

TANU imefanya kazi kubwa sana. Tulipopata uhuru tulikuwa ni mjumuiko tu wa makabila na kila kabila lilikuwa linajiona ni bora kuliko kabila lingine. Imekuwa hivyo katika nchi nyingi sana.

Baada tu ya uhuru, TANU ilichukua hatua za kuondoa tatizo hilo. Unaona hata Machief waliondolewa ili kusiwe na vikundi vya kikabila. Kikswahili kikafanywa kuwa lugha ya taifa. Zilifanyika jitihada za kuondoa udini. Hata shule za madhehebu ya dini zilitaifishwa.

TANU iliondoa tofauti za kikabila, udini na ubaguzi wa rangi. Wananchi wote tukawa sawa na wamoja na kufanya hivyo kulijenga uzalendo.

Uzalendo wetu ulizaa umoja wa kitaifa na umoja ukaleta amani. Uwepo wa amani ni hatua kubwa sana iliyopigwa na taifa. Huwezi kufanya shughuri zozote za kimaendeleo kama huna uhakika wa amani.

Taifa limepiga hatua kubwa sana kwenye kuondoa ujinga, maradhi na umasikini. Kuondoa ujinga, maradhi na umasikini ni mchakato endelevu.

Jaji Warioba: Mimi nimefanya kazi kwenye awamu ya Mwl. Nyerere chini ya Mawaziri Wakuu wanne. Mzee Kawawa, Marehemu Sokoine, Mzee Msuya na Dk. Salim. Mtu akiniambia kuwa hawa hawakufanya lolote, yaani tusahau historia yetu.

Mzee Kawawa utamuweka wapi hasa ikichukuliwa alikuwa anaitwa simba wa vita kwa kazi aliyokuwa anafanya. Nani anaweza kuwa kasahau aliyofanya Marehemu Sokoine?. Ukifanya hivi utakuwa unadanganya wananchi. Walifanya mengi kwa kiwango cha wakati ule na ndiyo umekuwa msingi wa kuendeleza.

Kazi zao zilitujengea taasisi za serikali, mashirika ya umma, ulinzi na usalama ambazo tunajivunia kwa sasa. Ni kweli taasisi zitakuwa na mtikiso wa hapa na pale kwa sababu ya mabadiliko mbali mbali.

Yusuf Kamote: Unalionaje suala la rushwa nchini.
Jaji Warioba: Rushwa imeanza kuwepo tokea kwenye awamu ya kwanza ya Mwl. Nyerere ambapo katika awamu ya pili kulifikia hatua ya Baraza lote la Mawaziri kujiudhuru kutokana wizara nyingi kukabiliwa tuhuma za rushwa. Mimi nilikuwa Waziri Mkuu.

Wakati tunaenda kwenye uchunguzi kufahamu vyanzo vya rushwa, wananchi wengi hawakuamini kama kuna rushwa nchini. Wananchi wengi walidhani rushwa ipo kwenye nchi kama Nigeria na Kenya. Repoti yetu ile imetumika katika nchi nyingi duniani.

Kwa sasa rushwa imekuwa kubwa zaidi mpaka imeingia kwenye siasa. Mpaka sasa imekwenda kwa wananchi wa kawaida wanategemea rushwa. Hata kwenye uchaguzi ndani na nje ya vyama kwa sasa rushwa inatumika. Wajumbe hawaogopi kuomba rushwa kwa wagombea.

Hizi rushwa kubwa zaidi ndiyo zinafanya mapato yetu kitaifa yasitumike kwenye maendeleo ya wananchi wote. Kwa kweli kama taifa inabidi tubadilike.

Mimi sitaki kusemea wengine lakini sisi wanachama wachache ambao tuliomba CCM kisiteue mtu ambaye anatumia msingi wa fedha nyingi katika uchaguzi ili chama kifanye mabadiliko na kuanza safari ya kujiunda upya. Kama mgombea anatumia msingi wa fedha nyingi lazima atakuwa na watu wanaompa fedha ambao ni matajiri wakubwa wanaotegemea kuzirudisha kwa njia yoyote. Kama nilivyosema, kiongozi akiwa na uhusiano na matajiri wakubwa, huo ndiyo msingi wa ufisadi.

Tuliomba pia chama kisiteue mwanachama ambaye ana makundi kwa sababu makundi nayo yanatumia fedha nyingi na nikichocheo cha rushwa.

Kwa kweli chama katika uteuzi huu kimefanya kazi nzuri. Hata ninyi waandishi wa habari mnajua jinsi ilivyokuwa wakati wa kusaka udhamini ndani ya CCM. Mliona yale makundi yalivyokuwa.

CCM ilimteua mwanachama ambaye hakutumia fedha nyingi na hakuwa na makundi. Kwa sasa kwa huyu tuliyenae ninaamini yuko tayari kupambana na rushwa ndogo na kubwa kubwa.

Kuna watu wanafikiri unaweza kuimaliza rushwa kwa kutumia TAKUKURU. TAKUKURU ni chombo kidogo sana hasa kama Rais atakuwa hana maadili. TAKUKURU haiwezi kushughulikia viongozi kwa matendo yao.

Tunataka Rais mwenye dhamira ya kweli katika kupambana na rushwa na ufisadi. Chanzo cha matatizo nchini kwa kiasi kikubwa ni rushwa na ufisadi. Hata kwenye Tume ya Katiba Mpya tulisisitiza sana uwepo wa amani na maadili.

By MsemajiUkweli/JF