Ticker

10/recent/ticker-posts

Tanzania na Namibia wajadiliana Kuhusu SACREEE

Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu( Kulia) na Naibu Waziri wa Nishati wa Namibia, Kornelia Shilunga( kushoto), wakiwa katika picha ya pamoja na ujumbe kutoka Namibia na Watendaji wakuu wa Wizara ya Nishati baada ya majadiliano ya pamoja kuhusu Kituo cha Nishati Jadidifu na matumizi bora ya Nishati cha nchi zilizo Kusini mwa Afrika (SACREEE) katika Ofisi ya Wizara ya Nishati Dodoma.
Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (kushoto) akiongoza majadiliano ya pamoja na Ujumbe kutoka Namibia na Watendaji wakuu wa Wizara ya Nishati kuhusu Kituo cha Nishati Jadidifu na matumizi bora ya Nishati cha nchi zilizo Kusini mwa Afrika (SACREEE) katika Ofisi ya Wizara ya Nishati Dodoma.

Na Zuena Msuya, Dodoma.

Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu na Naibu Waziri wa Nishati wa Namibia, Kornelia Shilunga pamoja na ujumbe wake, wamekutana na kujadili kwa pamoja kuhusu Kituo cha Nishati Jadidifu na matumizi bora ya Nishati cha nchi zilizo Kusini mwa Afrika (SACREEE).

Mgalu alikutana na ujumbe huo, Desemba 2, 2019, uliofika katika Ofisi za Wizara zilizopo jijini Dodoma, kwa lengo la kuisisitiza Tanzania kuweka saini katika mkataba wa makubaliano ya pamoja yaliyofikiwa na Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika( SADC) juu ya kuanzishwa kwa SACREEE.

Katika mazungumzo hayo, Mgalu aliueleza ujumbe huo kuwa mpaka sasa Tanzania bado haijasaini Mkataba wa Makubaliano ya pamoja ya utekelezaji wa kituo hicho hadi pale uamuzi wa kuanzishwa kwa kituo hicho utakapoidhinishwa na Marais wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika( SADC).

Aidha, Mgalu alisema baada ya kukamilika kwa taratibu za kisheria juu ya uanzishwaji wa SACREEE, Tanzania iko tayari kusaini mkataba kwa ajili kuwezesha kituo hicho ambacho Makao yake Makuu yako nchini Namibia.

Halikadhalika, Mgalu alisema kuwa Tanzania na Namibia ni nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika(SADC), ni dhahiri Kwamba nchi hizo zitakuwa zikishirikiana kwa namna moja ama nyingine katika masuala mengine mbalimbali kupitia umoja huo.

Sambamba na hilo alisema nchi hizo pia zinaweza kushirikiana kwa kuuziana umeme kupitia njia ya kusafirisha umeme wa kV400 inayojengwa kwa ajili ya kuunganisha gridi za Tanzania na Zambia(TAZA) kwakuwa nchi hizo ni wanachama wa Mtandao wa Southern Africa Power Pool (SAPP)ambao uko chini ya SADC.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Namibia, Shilunga aliishauri kwamba Tanzania isaini mkatba huo ili SARCEEE isonge mbele kwa manufaa nchi wanachama pia alisema Namibia inaendelea kuhamasisha nchi zilizobaki zisaini mkataba huo.

Tayari nchi 8 kati ya 16 zimekwisha kusaini Mkataba wa makubaliano ya pamoja ya nchi wanachama wa Jumuiaya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya kuanzishwa kwa SACREEE ambayo ilizinduliwa mjini Windhoek nchini Namibia, Oktoba, 2018 na kuhudhuriwa na Mawaziri kutoka nchi wanachama wa SADC na Wakuu wa Taasisi za Kimataifa na Kikanda zinazohusika na sekta ya nishati.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2Yb9bRM
via

Post a Comment

0 Comments