Ticker

10/recent/ticker-posts

Jaji Mkuu wa Zanzibar, THBUB kushirikiana kutatua kero za wananchi

Jaji Mkuu wa Mahakama Kuu, Zanzibar, Omary Othman Makungu (kulia) akimsikiliza Mwenyekiti wa THBUB, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu aliyemtembelea ofisini kwake Desemba 2, 2019. Wa kwanza kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa THBUB, Mohamed Khamis Hamad.

Na Mbaraka Kambona.

Jaji Mkuu wa Mahakama Kuu, Visiwani Zanzibar, Omary Othman Makungu amemueleza Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu kuwa wako tayari kushirikiana tume kutatua kero za wananchi zinazohusu upatikanaji wa haki nchini.

Jaji Makungu alisema hayo alipokutana na Mwenyekiti wa tume ofisini kwake Visiwani Zanzibar Desemba 2, 2019. Makungu alitoa ahadi hiyo ya ushirikiano kufuatia Mwenyekiti wa tume kumuomba kusaidia katika kutatua malalamiko mbalimbali ya kudai haki yanayopelekwa tume kuhusu Mahakama.

Awali akitoa maelezo, Mwenyekiti wa tume alimwambia Jaji Makungu kuwa katika kazi zao wamekuwa wakipata changamoto nyingi zinazohusiana na Mahakama, hususani mahakama za mwanzo kuchelewa kushughulikia utoaji wa nakala za hukumu ya kesi, ucheleweshwaji wa kesi na mahabusu kukaa muda mrefu bila kesi zao kusikilizwa.

Jaji Mwaimu alimueleza Makungu kuwa wamekuwa wakipata sana malalamiko hayo na mara kadhaa wakiwasiliana na mamlaka husika ili kupata majibu kumekuwa na tabia ya kutojibu barua wanazowaandikia.

“Tunakuomba Mheshimiwa Jaji kwa huku Zanzibar utusaidie kwa hili, tunaomba ushirikiano wako ili wananchi wapate haki zao kwa wakati, maana tusiposhirikiana kutoa majibu kwa wakati inapelekea haki iliyostahili kuchelewa na inapoteza maana”alieleza Jaji Mwaimu Wakati akitolea ufafanuzi wa maelezo ya Mwenyekiti wa tume, Makungu alisema ni wazi kuwa Mahakama ni mdau mkubwa wa tume na hawana budi kufanya kazi kwa kushirikiana.

“Niwahakikishie tu, kuwa tutatoa ushirikiano kwa tume, imekuwa ni utaratibu wangu kila mwaka kutembelea Magereza, huwa nawachukua na mahakimu kwenda kusikiliza malalamiko ili wajue wanawajibu kiasi gani kwa wananchi”alisema Makungu “Ni lazima tufanye kazi vizuri, tushirikiane ili tuweze kuisaidia serikali, ni muhimu kuwa na makubaliano, inabidi tupange kikao kazi tukae kwa pamoja ili tuwekane sawa”alimaliza Jaji Makungu


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/35UrAoL
via

Post a Comment

0 Comments