Ticker

10/recent/ticker-posts

DC MCHEMBE AMPONGEZA RAIS MAGUFULI KWA KUMALIZA CHANGAMOTO YA MAJI NA KUINUA ELIMU GAIRO


Charles James, Michuzi TV

MKUU wa Wilaya ya Gairo, Siriel Mchembe amesema ndani ya miaka minne ya Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dk John Magufuli, Wilaya hiyo imepiga hatua kubwa kwenye miundombinu, elimu pamoja na sekta ya afya.

Akizungumza katika mkutano na Wananchi wa Wilaya hiyo, DC Mchembe amesema mwaka 2015 upatikanaji wa Maji ndani ya Wilaya hiyo ulikua chini ya asilimia 25 lakini kwa sasa upatikanaji umepanda na wanatarajia kufikia asilimia 60 ifikapo mwaka 2020.

Amesema tayari wameshapokea mashine ya kuchuja chumvi kwenye Maji ikiwa ni jitihada za Serikali kumaliza changamoto ya maji ambayo imekua ikiwakabili wananchi wa Wilaya hiyo.

" Ni wazi Rais Magufuli amefanya makubwa sana ndani ya Wilaya yetu ndani ya miaka yake hii minne, Sekta ya Maji peke yake tumepokea zaidi ya Bilioni 16. Tuna kila sababu ya kuishukuru Serikali yetu katika hili," Amesema DC Mchembe.

Akizungumzia sekta ya elimu ndani ya Wilaya hiyo amesema ndani ya miaka minne ya Dk Magufuli tayari wameshasajili Sekondari tatu na mwaka watasajili nyingine na hivyo kuwa na Shule za Sekondari 14 jambo ambalo wanaamini litakuza elimu lakini na kutekeleza ilani ya uchaguzi inayoelekeza kila Kata kuwa na shule ya Sekondari.

Kuhusu ufaulu amesema ndani ya miaka minne hii ufaulu pia umeongezeka kutoka asilimia 60 hadi 66 kwa Shule za Sekondari huku pia wakipokea zaidi ya Bilioni mbili ili za kutekeleza sera ya elimu bure.

" Tulikua na changamoto kubwa ya walimu wa Sayansi tunashukuru Serikali tayari ishatupatia lakini pia kupitia posho za Walimu Wakuu ambazo hazikuepo zamani tumepata zaidi ya Milioni 200 ambazo sasa kiukweli zimeongeza ufanisi na walimu wamepata ari ya ufundishaji jambo ambalo hakika linachangia kuongezeka kwa ufaulu wetu," Amesema DC Mchembe.

Kwa upande wa ufaulu wa Shule za Msingi umeongezeka kutoka asilimia 20 hadi kufikia asilimia 70 sambamba na kusajili Shule shikizi na wanakaribia kukamilisha ujenzi wa madarasa kwenye shule hizo ili waweze kuzipatia usajili wa kudumu.
 Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Mhe Siriel Mchembe akizungumza na Wananchi wa Wilaya hiyo kwenye mkutano uliofanyika katika uwanja wa CCM Gairo.
Wananchi wa Wilaya ya Gairo wakimsikiliza Mkuu wa Wilaya hiyo, Mhe Siriel Mchembe alipokua akizungumza nao ambapo alitumia mkutano huo kuelezea mafanikio yaliyofanywa na Rais Dk John Magufuli kwenye Wilaya hiyo ndani ya Miaka minne ya uongozi wake.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2Jz0jPZ
via

Post a Comment

0 Comments