Ticker

10/recent/ticker-posts

LOWASSA AIBUKIA KANISANI HANDENI IBADA YA KRISMASI......AWATAKA WATANZANIA WADUMISHE AMANI NA UPENDO..SOMA HII KAULI YAKE HAPA


Aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa ameibukia katika Kanisa la KKKT wilayani Handeni mkoani Tanga, kushiriki ibada ya Krismasi na kutumia nafasi hiyo kushukuru wapiga kura katika Uchaguzi Mkuu uliopita.

Wakati Lowassa akifanya hivyo, tayari Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ametoa agizo la kupiga marufuku mikutano ya walioshindwa uchaguzi, ikiwamo kushukuru kwa kuwa haina tija.

Lowassa alikuwa mgombea aliyeungwa mkono na muungano wa vyama vinne vya Chadema, NCCR-Mageuzi, NLD na CUF, vilivyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

Hata hivyo, kauli hiyo ya Majaliwa ilipingwa na chama cha Chadema, ambacho katika tamko lake kilisema inaonyesha namna CCM na Serikali yake vinavyoshindwa kuelewa kwamba kuna uhusiano kati ya dhana ya demokrasia ya vyama vingi na maendeleo.

Akiwa katika kanisa hilo, Lowassa alipopewa nafasi ya kusalimia waumini, alisema kuwa yeye ni muumini mwenzao na mara kwa mara amekuwa akienda kusali hapo kila anapopata nafasi, hivyo aliomba ushirikiano wa karibu.

Lowassa aliwashukuru  wale waliompa kura kwenye uchaguzi uliopita kwa nafasi ya urais na kuwataka kudumisha amani na upendo uliopo, kwani walikuwa na imani naye ndiyo maana walimpigia kura.

Pia aliomba kualikwa kwenye ufunguzi wa moja ya makanisa hayo ambayo utafanyika siku chache zijazo, akisema yeye tayari ni mwenyeji wa Handeni na atashiriki yale yote ambayo atashirikishwa.Lowassa aliwataka Watanzania kutumia amani kama silaha ya kujiletea maendeleo yao na ya taifa.

Lowassa yuko mapumzikoni na familia yake katika shamba lake la mifugo lililopo eneo la Mzeri huko Handeni, na aliwashukuru wakazi na wananchi kwa kudumisha amani baada kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu.

Alisema wingi wa kura walizompa yeye na wagombea wa Ukawa ni kielelezo cha namna walivyokuwa na imani kubwa kwao.

Awali, Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la KKKT  wilayani Handeni, Lewis Shemkala aliwataka Watanzania kumrudia Mungu kwa kubadilisha maisha yao kwao kufuata yale ambayo ameagiza kwa kuwa na roho ya imani na yenye huruma.

Shemkala alisema endapo watu watafuata miongozo ya kidini  kwa kukabidhi maisha yao kwa Mungu, hata mambo ya uharifu yatapungua nchini na wananchi wataishi kwa amani na utulivu kama zamani

Kwa upande wake mkazi wa mtaa wa Seuta na muumini wa kanisa hilo, Ndimmyake Mwakibinga, alisema wamefarijika kusali na kiongozi huyo mkubwa katika ibada hiyo.

Katika ibada hiyo wananchi wengi walionekana kumshangaa sana Lowassa badala ya kufuatilia ibada hali iliyoonyesha kuwa alikuwa kivutio kikubwa kwa waumini wa kanisa hilo.