Ticker

10/recent/ticker-posts

WAZIRI NAPE NNAUYE: NCHI ILIFIKA PAGUMU, TUMUOMBEE SANA MAGUFULI..MSIKIE ZAIDI HAPA


Waziri wa Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo, Nape Nnauye amesema Watanzania wanapaswa kumuombea Rais John Magufuli ili aendelee kutumbua majipu kwani nchi ilifika pagumu baada ya wezi kuonekana wajanja.

Akizungumza wakati akizindua tamasha la Krismasi lililofanyika katika Ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam Nape aliyemwakilisha Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan alisema haijalishi mafisadi nchini wamejenga mizizi kiasi gani, lazima majipu yote yatumbuliwe.

Alisema kila mmoja anatakiwa kuomba kwa imani yake kwani kazi aliyoifanya Rais Magufuli na anayotarajia kuendelea kuifanya sambamba na Baraza la Mawaziri na viongozi wengine ni kubwa. 

Nape alisema kazi ya kutumbua majipu siyo ndogo, kwani Dk Magufuli na jopo lake wanaamini kwamba Watanzania wana haki ya kufaidi matunda ya nchi yao.

''Nchi ilifikia hatua ngumu asiyeiba alionekana mjinga na mshamba na wezi walionekana wajanja, waliostaafu wakiwa maskini walionekana wajinga, muombeni Rais Magufuli atumbue majipu ili Watanzania wafaidi matunda ya nchi yao'', alisema Nape.

Alisema hakuna sababu kwa nchi kuendelea kuwa maskini, mwenye haki atapata haki yake huku kila mmoja akila kwa jasho lake na si vinginevyo. 

Waziri huyo ambaye aliimba pambio  liitwalo Yu Mwamba, alisema amani na utulivu wa nchi lazima viendelee na ili hayo yote yafanikiwe, Watanzania wanapaswa kuomba.

''Serikali tutahakikisha tunaitunza amani kwa gharama yoyote, hivyo viongozi wa Serikali na kidini wanapaswa kudumisha dhana hiyo ili nchi iendelee kuwa kisiwa cha amani, yapo mataifa yanatamani kuwa kama Tanzania lakini haiwezekani'', alisema Nape.

Nape alizindua albamu ya kwaya ya Wakorintho wa Pili kutoka Mafinga, Iringa na kuinunua kwa Sh1.5 milioni. Maaskofu na viongozi wa dini walifanya sala kwa dakika 15 iliyokuwa na lengo la kumwombea Rais Magufuli ili Mungu amlinde katika jitihada zake za kupambana na mafisadi.

Awali, Askofu David Mwasota alisema viongozi wa dini wanaunga mkono Serikali ya Awamu Tano kwa kutambua haki kwa Watanzania wote. 

''Tunampongeza Rais Magufuli kwa jitihada zake ambazo kwa muda mfupi amefanya mambo makubwa yanayoonyesha nuru kwa nchi yetu miaka mitano ijayo'', alisema Askofu Mwasota.