Ticker

10/recent/ticker-posts

Prof. Busagala: Hakuna athari Minara ya Simu Kujengwa Karibu na Makazi ya Watu asema

 Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), Prof. Lazaro                Busagala, akizungumza katika mkutano huo, leo Aprili 29, 2024. 

NA MAGENDELA HAMISI

MINARA ya simu kujengwa karibu na makazi ya watu hakuna madhara ya mionzi inayopatikana kwa wananchi kama ambavyo jamii nyingi imekuwa na hofu kutokana na kupata taarifa zisizo sahihi.


Hayo yamebainishwa Aprili 29, 2024 jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi  Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), Prof. Lazaro Busagala alipojibu swali baada ya kuwasilisha wasilisho katika kikao kazi mbele ya Wahariri na Waandishi wa Habari.


Katika wasilisho hilo ameweka wazi mafanikio ambayo yamepatikana katika kipindi cha Uongozi wa Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambapo wamepata mafanikio makubwa ikiwemo kufanya kaguzi nyingi na kuwa na ofisi 63 nchi nzima.


“Ofisi hizi 63 zinasaidia kufanya ukaguzi na udhibiti katika masuala ya nyuklia na kuwa na vifaa madhubuti vyenye thamani ya sh. billion 2.9 na kuwa na trela la kubebea mionzi linalosaidia wafanyakazi na wananchi kuwa salama,” amesema.


Amefafanua kuwa katika ofisi hizo kuna watumishi wenye mafunzo ya kuendesha mitambo na kutoa hudumu kwa kiwango kizuri katika maeneo yote na kuifanya nchi kuwa salama wakati wote.


Amesisitiza kuwa Watanzania wanatakiwa kuwa na imani Tume yao kwa maana inafanya kazi vizuri na vifaa ambavyo wanavyo vinawapa taarifa kila siku kuhusu masuala ya mionzi na kama kuna sehemu popote nchini kuna mwanya wa kuleta athari, mapema wanapata taarifa na kudhibiti.

 

Amesema katika utekelezaji wa Sheria ya Nguvu za Atomu Na. 7 ya 2003, Serikali imefanikiwa kusajili wataalam wa mionzi wenye sifa za kutoa huduma ya mionzi kwa wananchi hakuna tatizo katika eneo hilo.


Ameongeza kuwa katika miaka mitatu imesajili wataalamu 1,289 katika eneo la kutoa huduma ya mionzi kwa wagonjwa, kutengeneza, kukarabati na kuendesha vifaa vya nyuklia na hilo lilikuwa halifanyiki kwa kipindi cha miaka ya nyuma.


Aidha amesema katika udhibiti matumizi salama ya mionzi, Serikali imeongeza idadi ya wanaopewa lesseni kwa asilimia 102 kutoka leseni 297 kwa 2016/2017 hadi wastani wa 767 kwa mwaka.


Prof. Busagala amesemam kuwa, Serikali ya awamu ya sita imeondoa tozo na kupunguza tozo kwa kuamua kubeba gharama za upimaji (subsidy), hasa kwa wanaosafirisha bidhaa nje ya nchi kwa kupunguza kutoka asilimia 0.2 ya malipwani kuwa asilimia 0.1 ya malipwani, sawa na punguzo la asilimia 50.


Pia ameongeza kuwa mafanikio mengine ambayo wamepata ni kuwa na bajeti ya milioni 400 inayotolewa na Serikali kwa ajili ya kufanya tafiti na hadi zimefanyika tafiti 20 sanjari na utoaji elimu kwa wananchi.


Amesema mafanikio mengine ambayo yamepatikana chini ya uongozi wa Rais Samia ni kupeleka nje watumishi kuongeza elimu katika ya teknolojia na sayansi ya nyuklia kwa ngazi ya shahada za uzamili na kila mwaka watumishi watano wanapata fursa hiyo.




Post a Comment

0 Comments