SIKU zinakatika kama hazina akili nzuri. Mara mwisho wa mwaka
umeshasogea, saa hivi tutaanza kusikia zile nyimbo za mwishoni mwa mwaka
zinazoashiria ujio wa sikukuu ya Krismasi na Mwaka mpya.
Kuna
dhana imejengeka sana huku mitaani kuhusu uhusiano au ndoa na mtoto.
Watu wanaamini kuwa watoto wana nafasi kubwa ya kuongeza upendo katika
maisha ya wenza wawili. Kwamba ndoa isiyo na mtoto haiwezi kuwa imara na
yenye upendo.
Wanawake wamekuwa na imani kuwa kama hawana watoto katika ndoa zao,
basi mapenzi kutoka kwa waume au marafiki zao yanakuwa na mashaka ya
kuweza kustawi. Ni kutokana na sababu hii, wengi wamekuwa wakikimbilia
kwa waganga wa kienyeji wakiamini huko wanaweza kupewa mitishamba
itakayowawezesha kupata watoto wa kuimarisha ndoa zao.
Hili la waganga wa kienyeji litakuwa na siku yake rasmi ya
kulizungumzia, lakini leo ningependa kujikita kwenye swali hili la
msingi, kama ni kweli kwamba kuzaa mtoto katika ndoa au uhusiano
kunaongeza au kudumisha uhusiano wako.
Kibinadamu, mtoto ni zao ambalo kila mtu katika uhusiano angependa
liwepo, kwa sababu hata Mwenyezi Mungu alisema tuje kuijaza dunia.
Familia nyingi zinaishi kwa furaha zinapokuwa na watoto, kwani zinakuwa
na uhakika wa kuendelea kuwepo kizazi hadi kizazi!
Wapo wanawake wanaoishi kinyonge katika mahusiano mengi wakiwa hawana
amani kwa sababu ya kukosa mtoto. Wapo wengine wameshaachika kwa sababu
hiyo na wengi wengine wameendelea kutoa machozi kila kukicha kwa vile
tu Mwenyezi Mungu hakuwajaalia kupata mtoto.
Tunapozungumzia tafsiri halisi ya mapenzi baina ya wawili wapendanao,
suala la kupata au kutokupata mtoto haliwezi kuwa kigezo cha kupendana
kwao, vinginevyo labda waingie mkataba, kitu ambacho kimsingi siyo
mapenzi.
Mapenzi ni ile hali ya wawili kuishi ndani ya moyo mmoja, kwamba bila
uwepo wa mmoja wao, mwingine anakuwa katika wakati mgumu. Kila mmoja
anajihisi hajakamilika pasipo mwenzake, na hamu ya kuwa pamoja inabaki
kuwa ileile jana, leo kesho na siku zote.
Wapo
watu ninaowafahamu walioishi miaka zaidi ya 15 pasipo kupata mtoto,
lakini ukiwaona utafikiri wameanza kuishi jana, yaani penzi baina yao
halijifichi na mtoto hajawahi kuwa tatizo, ingawa mwanamke ni mtu
anayejisikia vibaya mno kwa kukosa mtoto.
Amani au uimara wa ndoa hauletwi na watoto, isipokuwa na namna jinsi
wawili walivyoamua kuishi. Zipo familia zilizo na watoto lakini maisha
yao ni ya kukatisha tamaa sana, kwa sababu kila siku ni ugomvi,
misuguano na presha tupu.
Mtu hawezi kuachana na mwenza wake kwa sababu ya mtoto, kwa vile
kwanza licha ya jambo hilo kuwa ni kudra za Mwenyezi Mungu, pia ni kitu
kinachozungumzika.
Watu wengi hudhani familia kukosa mtoto ni tatizo la mama pekee,
hawajui kuwa wapo hata wanaume ambao wana matatizo ya kushindwa
kusababisha ujauzito. Sasa katika uhusiano wa waliopendana kwa dhati,
watakaa na kujiuliza, nini chanzo?
Kimsingi, wanaweza kwenda kupata ushauri wa kitabibu kwa mabingwa wa
magonjwa ya uzazi. Kama mmoja wao ataonekana kuwa na tatizo, ni wazi
kuwa daktari atazungumza kama linatibika au la.
Lakini kama itathibitika kuwa ni tatizo ambalo haliwezi kutibika,
bado uwanja ni mpana kwa wapendanao kuamua, ama kukubaliana na hali hiyo
maisha yao yote, au kujitoa muhanga na kumruhusu mwenza mmoja
‘kuchepuka’ ili mradi tu kukidhi haja ya mtoto!
Kitu nilichogundua mimi, mwanamke anapokosa mtoto, kutokana na
kutojiamini, kila tatizo dogo linapotokea ndani ya nyumba, hukimbilia
kutoa madai ya kwamba hayo yote yanatokea kwa sababu ya kukosa kwake
mtoto!Nisisitize tu kuwa furaha katika ndoa au uhusiano wako iko ndani
ya mikono yako mwenyewe, mtoto ni kisingizio!