Ticker

10/recent/ticker-posts

CHAMA CHA CUF CHATANGAZA MKAKATI MZITO

cuf
CHAMA Cha Wananchi (CUF) kimesema kitakuwa tayari kuingia mitaani na kuungana na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Jaji Joseph Warioba, kupinga rasimu itakayopitishwa na Bunge Maalumu la Katiba kwa madai kuwa haitokani na mawazo ya wananchi.
 
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara ulioandaliwa na chama hicho wilayani Kaliua mkoani Tabora, Naibu Katibu wa CUF Tanzania Bara, Magdalena Sakaya, alisema CUF na vyama vingine vitamuunga mkono Jaji Mstaafu Warioba, kupinga rasimu ambayo haikutokana na maoni ya wananchi.
 
Alisema rasimu hiyo inayopendekezwa si ya Watanzania, bali ni rasimu ya Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba Samuel Sitta, Mwenyekiti wa Kamati ya Uandishi, Andrew Chenge, Ummy Mwalimu na Kamati zao ambazo kwa makusudi wameamua kuchakachua maoni ya wananchi na kuingiza yale wayatakayo wao kwa maslahi yao binafsi na familia zao.
 
Alisema vitu muhimu vyote wameviondoa ikiwemo uwazi na uwajibikaji, kutokuwepo kwa mikataba ya usiri ambayo inaliangamiza Taifa kila kukicha, lakini pia kuwawajibisha viongozi wakiwemo wabunge pale wananchi wanapoona hawawajibiki ipasavyo.
 
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chama hicho, Abdul Kambaya, alisema Mungu hakupenda Watanzania wawe maskini, bali ni kutokana na mfumo mbovu wa uongozi unaowekwa na CCM ndio unaleta umaskini mkubwa miongoni mwa jamii.
“Kuna vigezo vikuu vitatu vya umaskini na hili halihitaji kuwa na elimu ya kidato cha nne wala sita, ukiona unakula chakula usichokipenda ujue wewe ni maskini, ukivaa nguo usizozipenda ujue wewe ni maskini, lakini pia uangalie unapolala je, pana hadhi ya binadamu kuishi au kulala, ukiona una hali hiyo, wewe ni maskini,”alisema Kambaya.
 
Alisema rasilimali za nchi hii ikiwemo mbuga za wanyama, madini, maziwa, mito, bahari na sasa gesi ambayo yanakwenda sambamba na upatikanaji wa mafuta yanatosha kabisha kuondoa umaskini lakini ni vigumu kumwambia mtu anayeipenda CCM akakuelewa wakati nayeye ni mmoja wa watu wanaoathirika.
 
“CCM wanatugombanisha maskini kwa maskini, wao wako pembeni kwani haiwezekani polisi wawapige watu eti kwa sababu wanadai haki zao wakati na wao wenyewe ni maskini…tunapigania haki sawa kwa wote ikiwemo hata mafao ya uzeeni, lakini polisi hawa hawaoni hilo zaidi ya kutupiga ili watu wasidai haki zao,”alisema Kambaya.

Post a Comment

0 Comments