CHAMA
Cha Wananchi (CUF) kimesema kitakuwa tayari kuingia mitaani na kuungana
na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Jaji Joseph Warioba,
kupinga rasimu itakayopitishwa na Bunge Maalumu la Katiba kwa madai kuwa
haitokani na mawazo ya wananchi.
Akizungumza
kwenye mkutano wa hadhara ulioandaliwa na chama hicho wilayani Kaliua
mkoani Tabora, Naibu Katibu wa CUF Tanzania Bara, Magdalena Sakaya,
alisema CUF na vyama vingine vitamuunga mkono Jaji Mstaafu Warioba,
kupinga rasimu ambayo haikutokana na maoni ya wananchi.
Alisema
rasimu hiyo inayopendekezwa si ya Watanzania, bali ni rasimu ya
Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba Samuel Sitta, Mwenyekiti wa Kamati
ya Uandishi, Andrew Chenge, Ummy Mwalimu na Kamati zao ambazo kwa
makusudi wameamua kuchakachua maoni ya wananchi na kuingiza yale
wayatakayo wao kwa maslahi yao binafsi na familia zao.
Alisema
vitu muhimu vyote wameviondoa ikiwemo uwazi na uwajibikaji, kutokuwepo
kwa mikataba ya usiri ambayo inaliangamiza Taifa kila kukicha, lakini
pia kuwawajibisha viongozi wakiwemo wabunge pale wananchi wanapoona
hawawajibiki ipasavyo.
Kwa
upande wake Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chama hicho, Abdul
Kambaya, alisema Mungu hakupenda Watanzania wawe maskini, bali ni
kutokana na mfumo mbovu wa uongozi unaowekwa na CCM ndio unaleta
umaskini mkubwa miongoni mwa jamii.
“Kuna
vigezo vikuu vitatu vya umaskini na hili halihitaji kuwa na elimu ya
kidato cha nne wala sita, ukiona unakula chakula usichokipenda ujue wewe
ni maskini, ukivaa nguo usizozipenda ujue wewe ni maskini, lakini pia
uangalie unapolala je, pana hadhi ya binadamu kuishi au kulala, ukiona
una hali hiyo, wewe ni maskini,”alisema Kambaya.
Alisema
rasilimali za nchi hii ikiwemo mbuga za wanyama, madini, maziwa, mito,
bahari na sasa gesi ambayo yanakwenda sambamba na upatikanaji wa mafuta
yanatosha kabisha kuondoa umaskini lakini ni vigumu kumwambia mtu
anayeipenda CCM akakuelewa wakati nayeye ni mmoja wa watu wanaoathirika.
“CCM
wanatugombanisha maskini kwa maskini, wao wako pembeni kwani
haiwezekani polisi wawapige watu eti kwa sababu wanadai haki zao wakati
na wao wenyewe ni maskini…tunapigania haki sawa kwa wote ikiwemo hata
mafao ya uzeeni, lakini polisi hawa hawaoni hilo zaidi ya kutupiga ili
watu wasidai haki zao,”alisema Kambaya.
0 Comments