Ticker

10/recent/ticker-posts

Mhandisi Victor Seff asema TARURA imejipanga kuongeza nafasi za wahandisi wanawake,Mativila aipa kongole.

Mtendaji Mkuu  wa wakala wa barabara za Vijini na Mijini (TARURA) Mhandisi Victor H. Seff  akizungumza na wanahabari mjini Unguja Zanzibar jana

Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) umejipanga kuhakikisha kwamba wanaongeza nafasi za wahandisi wanawake kwa kuwajengea uwezo ili kuona wanashika nafasi za juu za uongozi katika idara mbalimbali za taasisi hiyo ili kuleta ufanisi wa kazi na utekelezaji wa majukumu waliyokabiliwa na taifa.

Hayo yamesemwa na Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Mhandisi Victor H. Seff wakati alipozungumza na waandishi wa habari katika hoteli ya Golden Tulip, Zanzibar wakati wa ufunguzi wa mkutano wa 8 wa wahandisi wanawake nchini.

Alisema mchango wa wanawake katika sekta mbalimbali nchini hivi sasa ni mkubwa ambapo msukumo maalumu unahitajika kuona kundi hilo linashiriki kikamilifu katika ujenzi wa taifa na kuleta maendeleo.

Alisema kwa sasa wapo jumla ya wahandisi 40 wanawake katika taasisi hiyo wakifanya kazi katika mikoa 26 ya Tanzania Bara ambapo wote kwa ujumla wameonesha ufanisi mzuri wa utekelezaji wa majukumu yao.

Alizitaja hatua wanazozichukuwa kwa sasa ni pamoja na kuwahamasisha kuwapa moyo zaidi ya kujiendeleza katika kozi mbalimbali ili waweze kwenda kufanya kazi na kuchukuwa nafasi katika maeneo mbalimbali ikiwemo mikoani.

"Kwa mfano bado nafasi nyingi za ngazi za umeneja katika mikoa mbalimbali zinashikiliwa na wanaume ambapo kwa sasa wamejipanga vizuri kutoa msukumo unaostahiki kwao", alisema.

Mapema Mhandisi Seff alisema TARURA inaendelea na kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria ikiwemo kuzifanyia matengenezo barabara zilizopo vijijini ili kupitika na wananchi kufanya shughuli zao za maendeleo.

Alisema kwa kushirikiana na wadau katika ujenzi wa barabara wamefanikiwa kujenga zaidi ya barabara zenye urefu wa kilomita 144,000 zikijumuisha barabara za wilaya kuweza kutumiwa na wananchi na kurahisisha shughuli za maendeleo.

Naibu Katibu Mkuu OR-TAMISEMI Mhandisi Rogatus Mativila akipata maelezo ya kazi mbalimbali za TARURA kutoka kwa Wahandisi Bi.Roziana Saki na Ngeleja wa Tarura walioshiriki katika mkutano huo

Naye Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI anayeshughulikia miundombinu Mhandisi Rogatus Mativila ambaye pia ameshiriki katika mkutano huo amesema wao kama Wizara wanaipongeza TARURA kwa kuwa na nia ya dhati ya kuhakikisha wanawapa nafasi na kuwajengea uwezo zaidi wahandisi wanawake ili waweze kuwa katika nafasi muhimu za maamuzi hivyo wizara itatoa ushirikiano kwa ajili ya kuisaidia TARURA katika kufikia lengo hilo.

Mhandisi Roziana Saki  wa TARURA  akitoa maelezo ya kazi mbalimbali za wakala huo kwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt.Hussein Ali Mwinyi aliposhiriki katika mkutano wa  waandisi wanawake nchini Mjini Unguja Zanzibar jana

Katika maonesho hayo Rais wa Zanzibar Dk.Hussein Ali Mwinyi akifuatana na viongozi wa serikali alipata nafasi ya kutembelea banda la Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) na kupata maelezo mbalimbali yanayohusu utekelezaji wa majukumu ya Wakala.

Post a Comment

0 Comments