Ticker

10/recent/ticker-posts

NAIBU WAZIRI OLE NASHA ATAKA TAFITI ZINAZOFANYWA ZIJIBU CHANGAMOTO ZILIZOPO KWENYE JAMII

Naibu Waziri Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha amesema tafiti zinazofanyika nchini zinatakiwa kujibu changamoto zinazoikabili jamii ya watanzania na Afrika kwa ujumla.

Naibu Waziri Ole Nasha ameyasema hayo Jijini Arusha
akifungua Mkutano wa kumi wa Kimataifa wa Jumuiya ya Watafiti katika Malighafi Afrika (AMRS- 2019) kwa niaba ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe Samia Suluhu Hassan.

Kiongozi huyo amesema Tanzania imejikita katika ujenzi wa uchumi wa  kati kupitia  viwanda hivyo ni lazima tafiti zinazofanyika zijikite kwenye maeneo ya sayansi, teknolojia na ubunifu ili zitumike kuimarisha utengenezaji bidhaa na huduma zinazoendana na azma hiyo.

“Ni nani anaamua nini kifanyiwe tafiti, je tafiti hizo ni za kuwafaidisha waliopo nje ya nchi au watanzania? ni lazima tujikite kwenye tafiti zitakazosaidia kutatua changamoto zilizopo katika mataifa yetu na hivyo sisi wenyewe  tuwe waanzilishi wa ajenda ya utafiti kulingana na mahitaji,” alisema Naibu Wazirii Ole Nasha

Kwa upande wake Rais wa Jumuiya ya Watafiti katika Malighafi ambae pia ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela, Prof. Hulda Swai amesema mkutano huo pamoja na mambo mengine utaainisha na kujadili maeneo ya vipaumbele vya tafiti ambavyo vitatumiwa na Vyuo Vikuu pamoja na Taasisi za kitafiti.

Akizungumza katika Mkutano huo Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. James Mdoe ametoa changamoto kwa wajumbe wa AMRS kuja na suluhisho la namna bora ya kutumia  vizuri utajiri wa malighafi zilipopo Afrika  kwa ajili ya maendeleoya Bara la Afrika.

Nae Makamu Mkuu wa Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Prof Emmanuel Luoga amesema kufanyika kwa mkutano huo katika chuo cha NM-AIST ni moja ya mambo muhimu katika kukuza uwezo wa Chuo kufanya tafiti zinazokidhi mahitaji ya kitaifa na kimataifa.

“Wote mnafahamu kuwa Chuo hiki kina hadhi ya Kimataifa, kwa hiyo wanapokuja wageni wa aina hii kupitia majadiliano yao wanasaidia kuongeza ujuzi mpya katika masuala ya tafiti ikiwa ni pamoja na kukuza mashirikiano baina ya Taasisi hizi,” alisema Prof. Luoga

Mkutano wa Kimataifa wa Jumuiya ya Afrika ya Watafiti katika Malighafi unafanyika kwa siku nne Jijini Arusha kuanzia Desemba 10, 2019 ikiwa ni mara ya pili kufanyika nchini tangu ilipoanzishwa mwaka 2000, na unakutanisha zaidi ya watafiti 300 kutoka nchi 36 ulimwenguni.
 Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi  na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa kumi wa Kimataifa wa Jumuiya ya Watafiti katika Malighafi jijini Arusha
 Rais wa Jumuiya ya Watafiti katika malighafi   Afrika Prof. Hulda Swai akielezea wajibu, malengo, mafanikio na matarajio ya Jumuiya hiyo wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa kumi wa jumuiya hiyo.
 Baadhi ya Wajumbe wa Mkutano wa kumi wa Kimataifa wa Jumuiya ya Watafiti katika Malighafi wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknoloji Mhe. William Ole Nasha wakati wa ufunguzi wa Mkutano huo.
 Makamu Mkuu wa Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Prof. Emmanuel Luoga akielezea kuhusu malengo na shughuli zinazotekelezwa na Chuo hicho wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa kumi wa Jumuiya ya watafiti katika Malighafi  unaoendelea chuo hapo.
 Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiwa katika picha ya pamoja na watafiti wakiwa na wadau mbalimbali wa tafiti. Mstari wa mbele  kushoto kwake ni Rais wa Jumuiya ya Watafiti katika Malighafi na kulia kwake ni Naibu Katihu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi  na Teknolojia Prof. James Mdoe akifuatiwa na Makamu Mkuu wa Chuo cha NM-AIST Prof. Emmanuel Luoga.



from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2PA3A3z
via

Post a Comment

0 Comments