Ticker

10/recent/ticker-posts

TAZAMA MASTAA WAKIJIACHIA MBELE YA RAIS JK...RAHA TUPUUU

Mwandishi wetu
Acha kabisa! Baadhi ya mastaa wa sinema na muziki Bongo, wamejiachia na kujikuta wakikata mauno mbele ya Rais Dk. Jakaya Mrisho Kikwete aliyekuwa mgeni rasmi aliyeambatana na Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro hali iliyozua minong’ono kwa waalikwa.
Tukio hilo lililoshuhudiwa na Ijumaa Wikienda lilijiri usiku wikiendi iliyopita kwenye Hoteli ya Hyatt Regency The Kilimanjaro ambapo kulikuwa na uzinduzi wa Kampeni ya Mama Ongea na Mwanao iliyoandaliwa na kusimamiwa na Msanii Wema Isaac Sepetu na Steven Mengere ‘Steve Nyerere’. Mwenyekiti wa kampeni hiyo, Steve Nyerere alianza kwa kuzungumzia lengo la Mama Ongea na Mwanao ni kuhakikisha kila mwanamama anaongea na mwanaye juu ya kupiga kura kwenye uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu. “Tutahakikisha kampeni hii inafika nyumba hadi nyumba, chumba hadi chumba ili kuona kila mzazi, hasa mama anaongea na mwanaye kwa sababu wanawake wana fursa kubwa ya kuongea na vijana wao na kuwahamasisha kupiga kura,” alisema Steve. “Mimi kama kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) najua ziwa la mama ni tamu na haliishi hamu, kampeni hii ina lengo la kufanya uamuzi na mabadiliko kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 hivyo kwa pamoja tunasema ushindi kwetu ni lazima,” alisema Wema ambaye ni makamu mwenyekiti wa kampeni hiyo. Kwa upande wake JK alianza kwa kuwatoa hofu wasanii waliokatwa kwenye kura za maoni na kuwaambia kuwa yeye alianzia hukohuko walikoanzia wao hivyo wasikate tamaa. “Nakumbuka mwaka 1995 na mimi nilikatwa lakini sikukata tamaa hadi 2005,” alisema JK akiunga mkono kampeni hiyo.
Baada ya uzinduzi huo, wasanii walimpa tuzo JK ambayo iliambatana na picha ya mke wake, Mama Salma Kikwete iliyotokana na kuiongoza vyema nchi hii na kumtakia mapumziko mema huku Migiro naye akipewa tuzo kisha wasanii wakaanza kula, kunywa na kukata mauno mbele ya kiongozi huyo wa nchi.
Imeandikwa na Shani Ramadhani, Musa Mateja na Imelda Mtema.