Ticker

10/recent/ticker-posts

MAMIA YA WANAFUNZI WA KITANZANIA WATIMULIWA KENYA......CHANZO KINADAIWA NI KISASI CHA KUHAMISHA WAHAMIAJI HARAMU WA KENYA


KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, mamia ya wanafunzi wa Kitanzania wanaosoma katika shule za msingi nchini Kenya, wameripotiwa kufukuzwa nchini humo.

Tayari 50 kati yao, wamerejeshwa nchini huku wengine kadhaa wakiwa bado wamekwama katika eneo la Narok Magharibi. Baadhi ya walioathirika ni wale ambao wako katika hatua za mwisho za kuhitimisha elimu yao ya msingi katika darasa la nane.

Vijana hao wanatarajiwa kufanya mitihani yao ya kumaliza shule Oktoba mwaka huu ; na kufukuzwa kwao kunawaweka katika wakati mgumu zaidi kimasomo.

Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Hashim Mgandilwa alikiri kuwepo na tatizo hilo na alilieleza gazeti hili jana kuwa: “Ni kweli wanafunzi wetu waliokuwa wanasoma Kenya wamefukuzwa nchini humo na 44 kati yao wamesharudi nchini, ila tuna wasiwasi kwamba mamia wengine watakuwa bado wamekwama huko na tuko mbioni kuwafuatilia zaidi.”

Meneja wa Baraza la Wafugaji katika Tarafa ya Ngorongoro, Peter Metele naye alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na kuongeza kuwa yeye ndiye
anayefanya kazi ya kwenda kuwachukua wanafunzi waliotimuliwa Kenya.

Imeelezwa kuwa chanzo cha kutimuliwa kwa watoto hao ni msuguano, ulioibuka baada ya kufanyika kwa operesheni maalumu ya kuwaondoa wahamiaji haramu kutoka nchi jirani ya Kenya, wanaodaiwa kuvamia maeneo ya Loliondo na Sale.

Hadi sasa watoto 27 wamehifadhiwa kwenye nyumba ya kulala wageni ya Cobra katika eneo la Wasso, Loliondo. Wengine takribani 10 wamepelekwa kwenye kata ya Arash na waliobakia wako majumbani mwao.

“Tumewahifadhi kwenye nyumba za kulala wageni kwa sababu kuna wale wanaotoka vijiji vya mbali sana na tunataka tujitahidi kufanya mazungumzo na viongozi wa upande wa Kenya ili waruhusiwe kurejea mashuleni, iwapo tutafanikiwa basi iwe rahisi kuwarudisha Kenya,” alisema Mwenyekiti wa Baraza la Wafugaji wa Ngorongoro, Metili.

Imedaiwa kuwa wanafunzi waliofanikiwa kurejeshwa ni wale wanaodhaminiwa na Baraza la Wafugaji na wale waliopelekwa na taasisi mbalimbali, ambao ilikuwa rahisi kutumiwa usafiri, ila kwa waliopelekwa na wazazi wao, bado wamekwama Kenya.

“Tulishafanya mazungumzo ya awali na viongozi wa upande wa Kenya siku ya tarehe 12 Mei mwaka huu, lakini ingawa tulikubaliana mengi, ikiwemo wafanyabiashara wetu kuruhusiwa kupeleka bidhaa Kenya inaonekana kuwa wananchi wa Narok wao wana maamuzi yao tofauti na serikali yao hivyo wanasisitiza kuendeleza mzozo, na sasa wameamua kuongeza tatizo kwa kuwatimua watoto,” alisema Mkuu huyo wa Wilaya.

Kwa upande wake, Katibu wa Baraza la Wafugaji, Ngorongoro, James ole Moringe alisema baraza hilo pia linafanya jitihada za kukutana na viongozi wa Narok na walimu wa huko ili kupata mwafaka wa suala hilo.

Akisimulia, mmoja wa wanafunzi hao, Lilian Peter (14) anayesoma darasa la Nane katika

Shule ya Ilkerin-Loita, alisema Chifu wa eneo hilo alifika shuleni kwao na kuwaita walimu ofisini, kisha baadaye Mwalimu Mkuu, Abel Githinji alianza kuingia madarasani na kuwatoa wanafunzi wote wa Kitanzania huku akiwaagiza wafungashe virago.

Wengi wa wanafunzi hao ni wale wanaotoka kwenye tarafa mbalimbali za wilaya ya Ngorongoro, ambayo imepakana moja kwa moja na Kaunti au Jimbo la Narok, Kenya.

Mwanafunzi mwingine, Naini Petey ambaye anasema wenzao wanaosoma shule nyingine ya Naikara, pia walifukuzwa na wengi wao bado wamekwama nchini Kenya, wakisubiri wazazi au wafadhili waende kuwachukua.

Juhudi za gazeti hili kuwapata mawaziri wenye dhamana ya mahusiano ya kimataifa, Bernard Membe wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Dk Harrison Mwakyembe wa Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki, hawakupatikana katika ofisi zao, kwa njia za simu na hata bungeni Dodoma kuweza kuzungumzia suala hilo.

Chanzo: Habari Leo

Post a Comment

0 Comments