Rais Jakaya Kikwete jana aliwaapisha
Katibu na Naibu Katibu wa Bunge Maalumu la Katiba, hali inayoonyesha
kuwa kazi ya Bunge sasa imeanza.
Walioapishwa ni Yahaya Hamisi Hamad ambaye anakuwa Katibu na Dk Thomas Kashilila anashika nafasi ya Naibu Katibu wa Bunge hilo.
Shughuli za kuapishwa kwa makatibu
hao, zilifanyika katika Viwanja vya Ikulu ndogo iliyoko eneo la Uzunguni
mjini Dodoma na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali.
Viongozi hao ni Waziri Mkuu Mizengo
Pinda, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Idd, Katibu Mkuu
Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, Mwenyekiti Mteule wa Bunge , Samuel Sitta
na Makamu wake Samia Suluhu Hassan.
Baada ya kiapo hicho, Rais Kikwete alikutana na Pinda, Sitta na Suluhu.
Hata hivyo mazungumzo yao yalikuwa ya faragha.
Akizungumzia nafasi yake Katibu wa
Bunge, Yahaya Hamad, alikiri kuwa kazi iliyoko mbele yake ni kubwa
lakini ana matumaini makubwa kwamba ataifanya kwa uadilifu mkubwa wa
hali ya juu.
Hamad alisema changamoto kubwa
anayoiona ni mwingiliano wa masilahi ya wanasiasa kwa sababu wengi
wametanguliza misimamo ya vyama.
"Mimi ningewashauri wanasiasa kuacha
kila kitu ili tuweze kufanya kazi ya watu iliyotuleta Dodoma, ili tuweze
kupata Katiba nzuri itakayodumu kwa muda mrefu. Wanasiasa lazima
wakubali kuwa nchi kwanza na vyama baadaye," alisema Hamad.
Kwa upande wake Dk. Kashillilah
alisema atatumia uzoefu wake kumshauri na kumsaidia katibu na wenyeviti
wa Bunge ili ndoto ya kuwa na Katiba nzuri itimie.
Hata hivyo, alikanusha madai kwamba Katiba Mpya haitapatikana kutokana na kelele za wanasiasa.
0 Comments