Ticker

10/recent/ticker-posts

Serikali yatoa mwelekeo Utatuzi wa Changamoto Mererani

Serikali kupitia Wizara ya Madini imesema inatambua changamoto  mbalimbali zinazowakabili wachimbaji wadogo wa Madini ya Tanzanite wilayani Simanjiro mkoani Manyara na ina mipango ya muda mrefu na muda mfupi wa  kuzitatua  changamoto hizo.

Hayo yamebainishwa jana Novemba 17,2023 na Waziri wa Madini *Mhe. Anthony Mavunde * wakati akizungumza na wachimbaji wadogo wa Madini ya Tanzanite , wafanyabiashara na wamiliki wa vitalu vya uchimbaji madini katika mkutano maalum ulioitishwa na Serikali ili kujadili changamoto zinazowakabili katika maeneo yao.


Mapema baada ya Mkuu wa Mkoa wa  Manyara Mh. Queen Sendiga kutoa taarifa , wachimbaji na wafanyabiashara ya madini ya Tanzanite walielezea juu ya changamoto walizonazo ikiwa pamoja na ukosefu wa Nishati ya Umeme katika migodi , mitobozano chini ya ardhi , ubovu wa miundombinu ya Barabara, kukosekana kwa minada ya kuuza madini , ukosefu wa maji na vituo vya afya, ukosefu wa mitaji ya kuendeleza uchimbaji na vifaa duni vya uchimbaji.

Akielezea kuhusu mikakati iliyopo ya kutatua changamoto hizo Waziri Mavunde amesema kuwa Serikali ipo katika hatua za mwisho za kupitia upya kanuni za masoko, uongezaji thamani na kanuni za  eneo tengefu la Mererani ili kufanikisha minada ya vito pasipo vikwazo.

Kuhusu Mitobozano , Waziri Mavunde amesema hakuna sheria inayoruhusu mitobozano katika uchimbaji madini kisheria leseni zote zina mipaka hivyo kila mchimbaji azingatie mipaka yake iliyopo katika leseni na kumtaka Afisa Madini Mkazi wa Mirerani kuhakiksha anakaa na wadau kutatua changamoto ili kuruhusu shughuli za madini ziendelee pasipo kuleta athari katika ukuaji wa sekta.

Akijibu hoja ya kuwepo kwa zahanati  katika mgodi , Waziri Mavunde ameeleza kuwa mpango wa Wizara ya Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ni kujenga  zahanati kumi na moja katika wilaya ya Simanjiro na zahanati moja  itajengwa ndani ya mgodi ili wachimbaji waweze kupata huduma ya haraka.

Akifafanua kuhusu uwezeshwaji wa mitaji na vifaa vya kufanyia kazi , Waziri Mavunde amesema tayari timu maalum imeishakaa na taasisi za fedha na Benki kuangalia namna bora ya kutoa mikopo kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini na kwasasa yapo maeneo ambao wameanza kunufaika na mkopo huu.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Manyara *Mh. Queen Sendiga * amemtaka Meneja wa TANESCO  wilaya ya Simanjiro ifikapo siku ya  jumatatu kupeleka mpango kazi wa usambazaji  umeme katika maeneo yanayohitaji huduma hiyo tofauti na ilivyo sasa ambapo sehemu kubwa ya Nishati ya  Umeme ipo katika eneo ambalo kwasasa bado hawaitaji huduma hiyo.


Naye, Mbunge wa Jimbo la Simanjiro *Mh. Christopher  Ole Sendeka * ameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa Dkt .Samia S. Hassan kwa kuwapelekea fedha za maendeleo katika sekta ya Afya , miundombinu ya Barabara ambapo sasa kuna  mpango wa ujenzi wa zahanati 11 ,ujenzi wa barabara ya kuelekea katika mgodi wa Mirerani  yenye urefu kilomita zaidi tano.

Ziara hii ilijumuisha pia Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Mh. Dkt. Suleiman Serera viongozi mbalimbali wa Serikali, Kisiasa pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama mkoani Manyara.

Post a Comment

0 Comments