Ticker

10/recent/ticker-posts

JE UNAHITAJI MPENZI WA MAISHA ?UKIFANYA HAYA UTAMPATA ANAYEKUFAA SOMA HAPA KIJANA NIKUJUZE

NI jambo la kumshukuru sana Mungu kwa wapenzi wasomaji wa XXlove kukutana tena, wiki iliyopita tulizungumzia juu ya hakuna haja ya kuhuzunika kwa kuachwa, bali jipe moyo kwa sababu utampata akupendaye. Leo napenda tujifunze namna ya kufanya ili kumpata atakayekufaa kama mwandani wako.

Miongoni mwa fumbo ambalo majibu yake huwa ni magumu kwa mwanadamu ni suala la kumpata mtu anayefaa katika uhusiano wa kimapenzi kama mume au mke.Kidunia ni ngumu sana kufumbua fumbo hilo lakini kwa Mungu ni jambo jepesi na rahisi sana.Kwanza kabisa kabla ya kutafuta atakayekufaa na kukupenda, wewe binafsi unapaswa kufanya yafuatayo;

Jiheshimu:
Lazima ujiheshimu kwanza wewe na wengine watakuheshimu tu bila kujali kipato, elimu, dini au jinsia yako, lakini kama utakuwa kinyume kila mtu atakuogopa na kukukwepa kujihusisha na wewe.

Jitambue:
Lazima ujitambue wewe ni nani? Unataka kuwa na familia ya mama au baba wa aina gani? Kama utajitambua basi familia yako itakuwa ni ya uzao wa kujitambua.

Jilinde:
Unapaswa ujilinde kitabia na hasa matendo yako kwa ujumla, ukiangalia vijana wengi sana wanajiingiza katika uhusiano wa kimapenzi wakiwa bado wadogo.Anayetaka mke au mume huwa anaangalia namna unavyojilinda ili hata kama akikufanya mke au mume hatakuwa na wasiwasi juu ya kukulinda kwani anajua unaweza kujilinda.

Acha umapepe:
Vijana wengi wanaonekana kuwa ni mapepe na wasiotulia ndiyo maana hata suala la ndoa ni gumu kwa kizazi cha sasa. Hii inasababishwa na vijana kurukaruka sana na kusahau kuwa kuruka huko kuna shida siku za usoni kama si magonjwa ya zinaa, utasa, ugumba basi kifo au kukosa mke au mume.

Kwa mtu anayetaka kuoa au kuolewa ni lazima huanza kwa kuichunguza familia ya muoaji na muolewaji kwanza kisha mlengwa na kama ikibainika hata wazazi wake walikuwa ni waluwalu basi hakuna muoaji au muolewaji.
Sidhani kama kuna mzazi anapenda mwanaye akateseke katika ndoa yake kama pengine alivyowahi kuteseka au kuona familia nyingine ikiwa katika hali hiyo.

Unaukumbuka wimbo wa “Manunga embe’’ ulioimbwa na Kundi la Zig Zaga Crew, kuna sehemu inasema “Wanawake wazuri wazuri wazuri wameolewa, yamebaki manunga embe yanahangaika’’ kimtazamo wimbo ule ulikuwa unazungumzia tabia nzuri ya mwanamke ndiyo inaweza kumfanya akapata mume, hata mwanaume vilevile.
Tukutane wiki ijayo katika sehemu ya pili ya mada hii.