Mkurugenzi
Mkuu wa ZIFF, Profesa Martin Mhando (wa pili kulia) akizungumza na
waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa kuzindua rasmi Tamasha la
Filamu la nchi za Majahazi la 17 maarufu kama Zanzibar International
Film Festival (ZIFF). Kulia Msaidizi wa Kitengo cha habari ZIFF, Lara
Prieston, Kushoto ni Meneja wa Tamasha la ZIFF, Daniel Nyalusi (Dean),
Afisa Mawasiliano wa ZIFF, Hassan Musa "Has T" (wa pili kushoto) na
Music Coordinator wa ZIFF, Edward Lusala (katikati).
Music
Coordinator wa ZIFF, Edward Lusala akisisitiza jambo wakati wa mkutano
na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusiana na wasanii watakaotoa
burudani kwenye tamasha hilo.
Picha na Zainul Mzige wa modewjiblog
*Geneviveve Nnaji na John Dumelo nao ndani
*Habib Koite, Didier Awadi kuburudisha
*Filamu ya Mandela kufungua pazia
Na Andrew Chale
DUNIA inatarajia kushuhudia tukio kubwa na la kihistoria ndani ya
viunga vya Ngome Kongwe ndani Mji Mkongwe wa Stone Town, Unguja, kwa
watu wa mataifa yote watakapoungana na kushuhudia ‘Hatma ya Pamoja’ (A
common Destiny) Juni 14 hadi 22, 2014, katika Tamasha la Kimataifa la
filamu la Zanzibar (ZIFF).
Tamasha hilo maarufu kama filamu la nchi za Majahazi ZIFF, kwa mwaka
huu linatarajiwa kufanyika kwa mara ya 17, tokea kuanzishwa kwake.
Akizungumza mapema leo jijini Dar es Salaam, kwenye halfa maalum ya
uzinduzi wa tamasha hilo la 17, kwa wandishi wa habari iliyofanyika
Goethe Institut kituo cha utamaduni, Mkurugenzi Mkuu wa tamasha hilo,
Profesa Martin Mhando, alisema tamasha hilo msimu wa mwaka huu
linatarajiwa kuwa moto kwani linakuja na mambo mbalimbali yenye kuleta
mabadiliko ya hali ya juu.
Ni kutokana na mabadiliko hayo, Profesa Mhando anasema tasnia ya
filamu kwa Tanzania inahitaji kubadilika ikiwemo wasanii wenyewe
kujituma na hata kuingia darasani ili kufanya kazi zenye uhakika.
Akimaanisha kila msanii wa filamu aweze kufikia malengo yake, hana
budi kujifunza na kushirikisha wale waliotangulia katika tasnia hiyo.
Anazungumziaje kaulimbiu ya ‘A Common Destiny’
Prof. Mhando amesema kauli mbiu ya mwaka huu yenye kusema Hatma ya
pamoja yenye maana ya ‘A common Destiny’, ina lengo la kuwakutanisha
watu wa mataifa mbalimbali kuwa kitu kimoja na kufurahia kwa pamoja
ikiwemo kubadilishana mawazo kwa pamoja kwa tasnia ya filamu, muziki,
kwa mlengo ya kujenga.
“Tukiwa na haja moja, kuishi kwa amani na kuleta mapinduzi ya
kiuchumi, kifikira na maendeleo kwa amani, ZIFF kwa kutumia dira hiyo
hasa kupitia filamu zetu za ndani zenye mchanganyiko wa utamaduni na
asili yetu.
“Wazanzibari na hata wageni watakaoshuhudia filamu hizi wataweza
kuchukua utamaduni huo na kuupeleka nje kwa furaha kubwa katika kufikia
hatma ya pamoja” amesema Prof. Mhando.
Tukio kubwa ambalo kwa sasa Tanzania hasa kwenye viunga vya Zanzibar
na nchi nyingine duniani katika tamasha hilo la 17, ni ujio wa msanii wa
Kenya na Mexico, Lupita Nyong’o, atakayeudhuria utoaji wa tuzo hizo za
ZIFF mwaka huu.
Lupita ambaye ametwaa tuzo za Oscar na nyingine nyingi na kupelekea
kutikisa Hollywood kwa sasa ni miongoni mwa mastaa watakaokuwa kwenye
tamasha hilo huku akitarajiwa kuambatana na wazazi wake wote wawili
pamoja na wadogo zake.
Prof. Mhando amesema tayari wazazi wote wawili wa Lupita akiwemo
Dorothy na Peter Anyang’ Nyong’o, watakuwapo kwa siku zote 10 kwenye
tamasha hilo huku Lupita mwenyewe akiahidi kuangalia uwezekano wa
kuhudhuria japo katika utoaji wa tuzo kama ratiba za shughuli zake
hazita mbana.
Prof. Mhando alisema Lupita ni zao la ZIFF na ndiyo iliyomfungulia
mwanya wa kujulikana na baadaye alienda kusoma zaidi masuala hayo ya
filamu, ambapo alishiriki ZIFF 2007 kama Volunteer.
Mara nyingi staa huyo amekua akihudhuria matamasha na halfa
mbalimbali za utoaji wa tuzo na zawadi zingine huku akiwa ameambatana na
wazazi wake wote wawili.
Lupita mbali na tuzo hiyo ya Oscar, kupitia filamu ya ‘12 Years a
Slave’ pia filamu hiyo imempatia tuzo mbalimbali zikiwemo: tuzo ya Steve
McQueen kama mwigizaji mwenye mvuto, mwigizaji bora wa kike
aliyeshirikishwa, ‘Academy Award’, ‘Screen Actors’ Guild Award’, ‘NAACP
Image Award’, ‘Independent Spirit Award’, ‘Broadcast Film Critics
Association Award’, na nyingine nyingi.
0 Comments