Ticker

10/recent/ticker-posts

WAZIRI KAMWELWE AZINDUA HUDUMA YA MAWASILIANO VIJIJINI MLELE

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe (mwenye suti ya bluu) akifurahi baada ya kukata utepe kuzindua mnara wa mawasiliano kwenye kijiji cha Kanoge kilichopo wilayani Mlele mkoani Katavi. Wa pili kushoto ni Mkuu wa Wilaya hiyo Rachel Kasanda na wa tatu kulia ni Justina Mashiba, Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote
Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, Justina Mashiba akitoa taarifa kwa wananchi wa kijiji cha Kanoge kilichopo wilayani Mlele mkoani Katavi (hawapo pichani) kuhusu ujenzi wa minara ya mawasiliano wilayani humo. Wa pili kulia aliyekaa anayesikiliza ni Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe (aliyesimama mbele) akiongea na wananchi wa kijiji cha Mgombe kilichopo wilayani Mlele mkoani Katavi kuhusu ujenzi wa minara ya mawasiliano na upatikanaji wa huduma za mawasiliano wakati wa ziara yake wilayani humo

*************************************

Na Prisca Ulomi-WUUM, Mlele

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Aloyce Kamwelwe amezindua huduma ya mawasiliano vijijini kwenye Wilaya ya Mlele mkoani Katavi .

Mhandisi Kamwelwe amefanya uzinduzi huo jana kwenye kijiji cha Kanoge kilichopo Kata ya Utende Wilayani Mlele mkoani Katavi kwa kuzindua mnara wa mawasiliano uliojengwa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) kwa kushirikiana na Kampuni ya Simu ya Vodacom Tanzania ambapo ujenzi wake umegharimu shilingi milioni 300.

Mhandisi Kamwelwe amesema kuwa tumekuwa na kampuni za simu ila hazikutaka kwenda vijijini bali kwenye maeneo yenye hela, ila Serikali imeanzisha Mfuko wa UCSAF na inatoa ruzuku kwa kampuni za simu ambapo nazo zinachangia kujenga minara vijijini ili kupeleka mawasiliano maeneo yasiyo na mvuto wa kibiashara.

“Na kwa vile leseni natoa mimi, sasa nazielekeza kampuni za simu nenda kijijini au mahali fulani ambapo hamna mawasiliano na hakuna mvuto wa kibiashara na wanakwenda ili kufikisha mawasiliano kwa wananchi,” amesisitiza Mhandisi Kamwelwe.

Pia, amewaambia UCSAF walete mawasiliano ya data na sio ya sauti tu kwa kuwa bila data wanafunzi hawataweza kusoma shuleni na wananchi pia wanataka data. “Ndio maana awali nilileta kompyuta 50 kwa shule za msingi na sekondari, sasa naleta umeme ili watoto waanze kucheza na kompyuta kwa kuwa sasa hivi Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ni uchumi.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya UCSAF, Dkt. Joseph kilongola alisema kuwa kwa kutumia Mfuko wa UCSAF wanahakikisha mawasiliano yanawafikia wananchi kwa kuwa kampuni za simu pekee haziko tayari kupeleka mawasiliano maeneo ya vijijini Mtendaji Mkuu wa UCSAF, Justina Mashiba amesema kuwa hadi sasa usikivu wa mawasiliano umefikia kiwango cha asilimia 94 ukilinganisha na asilimia 45 mwaka 2009 wakati UCSAF inaanzishwa.

Mashiba ameongeza kuwa UCSAF imetangaza zabuni za kujenga minara ya mawasiliano kwenye kata 252 nchini ambapo utekelezaji wa zabuni utakapokamilika usikivu wa mawasiliano utaongezeka na kufikia kiwango cha asilimia 96.

Amesema kuwa UCSAF itaendelea kuhakikisha kuwa shule za umma zinapata kompyuta kwa kuwa wanafahamu kuwa shule zetu zina ukosefu wa vifaa vya TEHAMA ili tuwe na watanzania ambao wanaweza kutumia vifaa vya TEHAMA

Amefafanua kuwa UCSAF inaratibu uendeshaji wa mafunzo ya TEHAMA kwa waalimu ili kuhakikisha kuwa waalimu wanakuwa na uelewa na ujuzi wa kutumia vifaa hivyo ili kuweza kuwasaidia wao kufundishia na wanafunzi kujifunzia ambapo tayari wameendesha mafunzo hayo kwa waalimu 72 wa Mkoa wa Katavi ambapo waalimu wane walitoka Mlele.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mlele, Rachel Kasanda aliwaambia wananchi kuwa hakuna mtoto atakayebaki bila kwenda sekondari baada ya wiki mbili kupita baada ya shule kufunguliwa tarehe 6 Januari mwaka 2020
“Watoto wote wawe wameripoti shuleni, vinginevyo mzazi jiandae kwa faini ya shilingi laki tatu na kifungo cha mwezi mmoja jela, kama mzazi umepokea mahari na kumuozesha mtoto au umempeleka mahali kufanya kazi, mrudishe, Serikali tunataka watoto wasome,” amesisitiza Kasanda
 
Mkuu wa Kanda za Nyanda za Juu Kusini wa Kampuni ya Vodacom, Ezekiel Nungwi amesema kuwa wako tayari kuendelea kushirikiana na Serikali kupitia UCSAF ili kuhakikisha kuwa wananchi wanawasiliana kidijitali kwa kujenga minara maeneo mbali mbali ya vijijini nchini kwa kuwa tayari kampuni yao imejenga mnara huo wenye uwezo wa kutoa huduma za mawasiliano ya data na sauti kwa wananchi wa kijiji cha Kanoge na maeneo yanayozunguka eneo hilo .

Naye mwananchi wa kijiji cha Kanoge, Cretus Edus amesema kuwa wanaishukuru Serikali kwa kujenga mnara huo kwa kuwa sasa wanafahamu mambo mengi kupitia mtandao ambapo zamani walikuwa wanasikia you tube, facebook ila sasa wanajua na wanafahamu.

“Zamani kupiga simu au kuweka vocha ilikuwa mpaka uende kwenye mti na ukiongea na simu hakuna siri kwa kuwa kila mtu anakuja hapo hapo ila kwa sasa unapiga simu hata ukiwa ndani,” amefafanua Edus.

Ameongeza kuwa sasa hivi tunafanya biashara kwa kutumia simu ya mkononi ambapo tunauza biashara ambapo nauza asali ya kutoka hapa Inyonga, Mlele kwenda Dar es Salaam kupitia mtandao wa simu.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2ZE7H3s
via

Post a Comment

0 Comments