Ticker

10/recent/ticker-posts

WIZARA YA ELIMU YAENDESHA MAFUNZO KWA WALIMU KWENYE HALMASHURI ZENYE UFAULU HAFIFU

Charles James, Michuzi TV

ILI kukuza kiwango cha ufaulu kwa baadhi ya Halmashauri hapa nchini, Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeandaa mafunzo maalum ya kwa walimu takribani 800 kutoka halmashauri 20.

Mafunzo hayo yanaratibiwa na wizara kupitia Mradi wa uwezeshaji wa elimu (TESP) kwa kushirikiana na ubalozi wa Canada ambapo kwenye hizo halmashauri 20 Shule za Msingi ni nane wakati za Sekondari zikiwa 12.

Akizungumzia mafunzo hayo mmoja wa wawezeshaji kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Dk Alfred Hugo amesema mafunzo hayo yaliyoanza Desemba 10 yatamalizika Desemba 23 na lengo likiwa ni kuwajengea walimu uwezo wa kutambua zana za kufundishia kulingana na mazingira.

" Tunaendesha mafunzo haya kwa walimu wa somo la hisabati kwa Shule za msingi na kwa Sekondari tumezingatia yale masomo ya Sayansi.

Mfano kuna changamoto kubwa ya ufundishaji kwa walimu hasa kwenye masomo ya Sayansi kwa kutokua na vifaa vya kufundishia lakini kupitia mafunzo haya wamejifunza mbinu mbalimbali za kuendana na mazingira waliyopo," Amesema Dk Hugo.

Amesema kupitia mafunzo hayo walimu wanafundishwa jinsi ya kuwa wabunifu kwenye ufundishaji ili kuwafanya wanafunzi kufurahia masomo na kutoona ugumu wowote hasa kwenye masomo ya Sayansi na Hisabati.

Kwa upande wake mmoja wa walimu walioshiriki mafunzo hayo kutoka Shule ya Msingi Banguma, Bi Nuru Mwendalile ameishukuru Serikali na ubalozi wa Canada kwa kuendesha mafunzo hayo ambayo anaamini yatakua msaada kwao pindi watakaporudi kufundisha.

" Tunaishukuru sana Serikali kwa kutuletea hii fursa. Ni kweli Wilaya yetu ina changamoto za ufaulu lakini tunaamini baada ya kupata mafunzo haya tutayatumia kuboresha kiwango chetu cha ufaulu kwa Shule zetu.

Tumejifunza kubadilika kutokana na mazingira tuliyopo, tumegundua pia hata kama tuna changamoto ya vifaa vya ufundishaji tunaweza kutumia majengo ya madarasa na vitu vingine vya asili kwenye mifano yetu tunapokua tunafundisha," Amesema Mwalimu Nuru.
 Mwalimu Nuru Mwendalile kutoka Shule ya msingi Banguma iliyopo wilayani Chemba mkoani Dodoma akizungumzia mafunzo ambayo yametolewa kwao na Serikali kupitia mradi uwezeshaji wa elimu TESP na ubalozi wa Canada.
Mwezeshaji wa mafunzo ya walimu kwa Shule 20 kutoka halmashauri ambazo zina ufaulu hafifu, Dk Alfred Hugo akizungumza na wandishi wa habari kuhusiana na mafunzo hayo ambayo yanaendeshwa kwa wiki mbili sehemu mbalimbali nchini.
 Walimu kutoka Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma wakiwa kwenye mafunzo maalum yanayotolewa na Serikali kupitia mradi uwezeshaji wa elimu TESP na ubalozi wa Canada kwa halmashauri 20 zenye ufaulu hafifu nchini.

 


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2tHBfkN
via

Post a Comment

0 Comments