Ticker

10/recent/ticker-posts

‘UBUNGE SI SAIZI YANGU’-RC MAKONDA


Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda.

Na Richard Mwaikenda

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema ‘ubunge si saizi yake’ kuliko cheo kikubwa alicho nacho cha ukuu wa mkoa.



RC Makonda amewananga watu ambao kila akifanya jambo la kimaendeleo ndani ya wilaya tano za mkoa huo, wana fikra potofu kwamba anafanya hivyo kwa lengo la kutaka kugombea ubunge 2020.



RC Makonda, aliyasema haya hivi karibuni alipokuwa mgeni rasmi katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi ujenzi wa jengo la kisasa la ghorofa moja la CCM Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam. Pia aliahidi kujenga majengo kama hilo katika wilaya za Ilala, Ubungo, Temeke na Kigamboni yatakayogharimu zaidi y ash. Bil. 2.



Alisema kuwa nafasi aliyonayo ya ukuu wa mkoa ni kubwa kuliko ubunge, kwani ana mamlaka makubwa kuliko hata wabunge  kumi waliopo katika mkoa anaouongoza.



Aidha, Makonda, amesema kuwa hata katika baadhi ya vikao au mikutano ya mkoa anayoongoza, wabunge hawawezi kuongea bila kupata ridhaa kutoka kwake.



“Kuna watu wana fikra potofu  wakiona ofisi inajengwa wataanza kufikiri cheo cha ubunge. Cheo nilichonacho ni kikubwa mno kuliko ubunge, mimi nikikaa kwenye kikao changu, wabunge wote kumi wanaomba  ruhusa ya kuongea kwangu,’alisema Makonda huku akishangiliwa na wana CCM waliofurika katika hafla hiyo.



“Maana yake nina majimbo yote kumi Dar,

Siamini kama kuna mwana CCM mzalendo ambaye anaweza kuhusisha kazi zangu na  ubunge wa jimbo moja.Wajibu wangu ni kuwatumikia wananchi wote bila kusahau CCM iliyomuweka madarakani Rais Magufuli,” alisema Makonda.



“Hizi nafasi zipo  na zinakuja kwa ratiba za Mwenyezi Mungu, lakini wajibu wangu ni kufanyakazi niliyopewa na Rais John Pombe Magufuli ya kuwatumikia wananchi wote bila kusahau chama kilichotuweka madarakani.”



“Msingekuwa nyie wana CCM, kusimama imara kutafuta kura; kukubali kutukanwa, kuzomewa na hata wengine kuvuliwa nguo mkipita maeneo mbalimbali ikiwemo  Kariakoo, lakini mlisimama imara kumpigania Rais John Magufuli, sasa ni wakati wenu wa kula matunda ya jasho lenu, wala mimi siwezi kukaa kwenye kiti na kusahau jasho mlilotoa, nakumbuka ugumu na jasho mlilotoa mwaka 2015,” alisema Makonda.



Aliwasihi wana CCM kuendelea kujenga umoja, mshikamano na uzalendo kwa CCM na kwamba ofisi anazojenga  ni alama  na kielelezo cha mapenzi  na utiifu wake kwa chama chake kilichomlea.



“Sina sababu ya kujificha, mimi si mteule ambaye anakionea haya Cha Cha Mapinduzi. Mimi ni mteule ambaye nafurahia na kuji-proud ya kwamba ni  zao la ccm,” alisema Makonda ambaye amelelewa na Umoja wa Vijana wa CCM.



Alisema kuwa tangu ateuliwe katika nafasi hiyo amefanya mambo mengi ya maendeleo, huku akitaja baadhi ya miradi kama; Ujenzi wa Jengo la upasuaji Hospitali ya Mwananyamala, Hospitali ya Chanika, Jengo la Uzazi Hospitali ya Amana Ilala, utengenezaji magari ya polisi, kugharamia matibabu ya watoto 200 wenye matatizo ya moyo.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2QgsqY5
via

Post a Comment

0 Comments