Ticker

10/recent/ticker-posts

SHILINGI BILIONI 1.8 ZA CHENCHI YA VIFAATIBA, DAWA,NA VITENDEA KAZI KUTUMIKA KWA MAENDELEO NA KUBORESHA HUDUMA BMC

Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya BMC ya jijini Mwanza, Profesa Abel Makubi, kulia akifungua moja ya makufuli yaliyofungwa kwenye moja ya  kontena la vifaa tiba ,dawa na vitendea kazi kati ya makontena sita, baada ya kuwasili nchini na kupokewa jana na uongozi wa hospitali hiyo.
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Katoliki  cha Sayansi za Tiba za Afya (CUHAS) Profesa Paschalis Rugarabamu (kushoto) akikata utepe kuashirikia kupokea makotena ya vifaa tiba, dawa na vitendea kazi vya Hospitali ya Rufaa ya Kanda,  Bugando (BMC) vilivyonunuliwa kwa sh. bilioni 1.2 baada ya kuwasili nchini kutoka China.Kulia ni Mkurugenzi wa   hosptali hiyo Profesa Abel Makubi.

Askari wa Usalama barabarani akiwaongoza maandamano ya watumishi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda , Bugando pamoja na wanafunzi wa Chuo Kikuu Katoliki cha Sayansi za Tiba na  Afya (CUHAS)  wakiadhimisha Siku ya Bugando Day jana.

Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda , Bugando (BMC) Dk. Fabian Massaga (mwenye kofia wa tatu kutoka kushoto) akitoa ufafanuzi wa kotena moja kati ya sita ya vifaa tiba na madawa baada ya kuwasili na kupokelewa na Vvongozi na watumsihi wa hospitali hiyo jana,  na watumishi.Wa tatu kutoka kulia mwenye suti ya michezo ni Mkurugenzi wa hospitali hiyo Profesa Abel Makubi.
****************************
 NA BALTAZAR MASHAKA, MWANZA
HOSPITALI ya Rufaa ya Kanda,Bugando Medical Centre (BMC) imesema fedha zaidi ya sh. bilioni 1 zilizobaki kwenye manunuzi ya vifaa tiba,madawa  na vitendeakazi zitatumika kwa shughuli za maendeleo na kuboresha huduma mbalimbali za hospitali.
Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo, Profesa Abel Makubi alisema jana wakati wa maadhimisho ya Siku ya Bugando (Bugando Day) muda mfupi baada ya kupokea moja ya makontena kati ya sita ya vifaa hivyo vilivyogharimush. bilioni 1.2 kati y ash. bilioni 3 zilizokuwa zimetengwa kwa ajili hiyo.
Alisema hospitali  ya BMC ilikuwa na changamoto ya vifaa tiba na dawa na hivyo kuzua malalamiko kutoka kwa wagonjwa jambo lililousukuma uongozi na menejimenti kutafuta suluhu ya changamoto hiyo ambapo walishindanisha kampuni mbalimbali ili kujua bei ya vifaa tiba na madawa kulingana  mahitaji kabla ya kuagiza.
 “Ili kupunguza chagamoto hiyo uongozi na menejimenti ya hospitali  tulikubaliana kutumia fedha za ndani kuagiza vifaa tiba, madawa, vitendea kazi na sare za watumishi kwa gharama ya sh. bilioni 1.2  kutoka nchini China na kuokoa kiasi kikubwa cha fedha, endapo tungenunua hapa nyumbani ingetugharimu sh. bilioni 3,”alisema Profesa Makubi.
Alisema  kununua madawa na vifaa tiba nje kwa gharama nafuu wameokoa fedha nyingi wanazokusanya na kutumia kidogo lengo likiwa ni kuboresha huduma za tiba kwa wananchi na vitasaidia pia changomoto ya hospitali nyingi za umma kwa sababu zina matatizo ya vifaa tiba.
Alishauri taasisi za umma kulinda na kutumia kidogo wanachopata ili wananchi wapate huduma bora kwa kununua vitendea kazi katika kuboresha huduma  na kuzifanya kuwa bora.
“Ili kukabiliana na changamoto ya vifaa ni kuboresha huduma wananchi watibiwe kwa vifaa bora na katika mazingira bora, si vifaa tu hata mahali wagonjwa wapolala, hilo ndilo BMC tumefanya,”alisema Profesa Makubi.
Mkurugenzi huyo wa BMC alisema baada ya kupata vifaa tiba vya kisasa vya vipimo na upasuaji wa kibingwa kutaharakisha utoaji wa huduma na kwa ufanisi zaidi, kutaokoa muda na majibu kupatikana haraka badala ya mgonjwa kusubiri kwa saa mbili.
Dk. Makubi alitaja miongoni mwa vifaa tiba walivyopata kuwa ni mashine 6 za Utra Sound na vifaa vya upasuaji ambavyo vitawezesha wagonjwa kuchunguzwa na kufanyiwa upasuaji kwa haraka zaidi na kupunguza malalamiko ya kuchelewa kuhudumiwa.
Aliwataka watumishi wa hospitali hiyo wakiwemo wanaohudumu kwenye hospitali za serikali kujituma zaidi kuwahudumia wananchi haraka na kwa ubora kwani hiyo ndiyo rai ya menejimenti ya BMC na watumie lugha safi kwa wagonjwa.
“BMC tunawathamani watumishi kwa kuwapa faraja waone utendaji wao unathaminiwa, hii itawatia moyo na hamasa, hivyo kuwafanya wajitume zaidi kwa wananchi na kuhakikisha wanapata huduma bora za kiwango,”alisema Profesa Makubi.
Awali Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji, Dk.  Fabian Massaga, alisema shilingi bilioni 1.8 kati ya bilioni 3 zilizookolewa kwenye ununuzi wa vifaa tiba na madawa zitatumika kwa maendeleo na kuboresha huduma mbalimbali za hospitali.
Alivitaja baadhi ya vifaa tiba ni vitanda, mashine sita za Utra Sound,vifaa vya upasuaji (operating set), madawa mbalimbali, kompyuta zitakazounganishwa na mfumo na kuondokana na madaktari kutumia majadala kwa ajili ya kumbukumbu za wagonjwa na sare za watumishi vyote vikigharimu sh. bilioni 1.2 fedha za ndani.
Aidha, katika hatua nyingine Profesa Makubi, alisema wanapoadhimisha  Siku ya Bugando Day mwaka huu lengo ni kuwakumbusha watumishi wa  Hospitali ya BMC  majukumu yao, kuonyesha umoja na mshikamano kati yao na watumishi wa Chuo Kikuu Katoliki cha Sayansi za Tiba za Afya (CUHAS).   
Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo cha CUHAS, Profesa Paschalis Rugarabamu,alisema wanashirikiana chuo na hospitali kujenga maadili na kuhimiza vijana kutimiza majukumu yao ya utoaji wa huduma za tiba kwa kuzingatia maadili ya kitaaluma ingawa ni kazi ngumu.
Pia wamepanua wigo wa taaluma nje ya BMC kwa kuwapeleka wanafunzi wa chuo hicho kujifunza kwenye maeneo tofauti licha ya matakwa ya mtaala wanafanya mazoezi katika mazingira halisi kwa kuzijengea uwezo wa elimu na huduma katika hospitali za Sekou Toure na Sengerema DDH.
Hospitali ya Bugando iliyojengwa mwaka 1967 kwa msaada wa Serikali ya Ujerumani Magharibi kwa ushirikiano na Uholanzi kupitia shirika moja la kikatoliki ambapo mwaka huu imeadhimisha miaka 52 na  ilifunguliwa, Desemb 3, 1971 na Rais wa Kwanza wa Tanzania, Mwalimu Julius K. Nyerere


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2El3LKZ
via

Post a Comment

0 Comments