Ticker

10/recent/ticker-posts

RMO SHINYANGA AZINDUA MPANGO MKAKATI WA RAFIKI SDO 2020/2024


Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume akikata utepe kuzindua Mpango Mkakati wa shirika la Rafiki SDO wa mwaka 2020/2024 wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa shirika la Rafiki SDO uliofanyika leo Jumapili Desemba 22,2019 katika ukumbi wa Karena hotel Mjini Shinyanga. Kulia ni Mkurugenzi wa Rafiki SDO Gelard Ng’ong’a, Kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi Rafiki SDO, Seif Hamad. Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume akizindua Mpango Mkakati wa shirika la Rafiki SDO wa mwaka 2020/2024.
Kushoto ni Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume akimkabidhi Mkurugenzi wa Rafiki SDO Gelard Ng’ong’a Mpango Mkakati wa shirika la Rafiki SDO wa mwaka 2020/2024.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume (katikati) akifuatiwa na Mkurugenzi wa Rafiki SDO Gelard Ng’ong’a na Meneja Miradi wa Rafiki SDO Eliud Lazaro (kulia),Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi Rafiki SDO Happiness Misael na Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi Rafiki SDO, Seif Hamad wakionesha Mpango Mkakati wa shirika la Rafiki SDO wa mwaka 2020/2024.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume akilipongeza shirika la Rafiki SDO kwa utendaji kazi wake mzuri.

Wadau na wafanyakazi wa shirika la Rafiki wakimsikiliza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume.
Mkurugenzi wa shirika la Rafiki SDO Gelard Ng’ong’a akielezea kuhusu Mpango Mkakati wa Shirika la Rafiki wa Mwaka 2020/2024.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume akipiga picha ya pamoja na wadau pamoja na wafanyakazi wa shirika la Rafiki SDO.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume akipiga picha ya pamoja na wadau pamoja na wafanyakazi wa shirika la Rafiki SDO.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume akipiga picha ya pamoja na wafanyakazi wa shirika la Rafiki SDO waliopatiwa vyeti vya utendaji kazi mzuri.


Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Shirika la Rafiki SDO limezindua Mpango Mkakati wa miaka mitano ‘Strategic Plan 2020/2024’ utakaojikita katika maeneo nane muhimu ikiwemo sekta ya afya,elimu,maji na usafi wa mazingira,masuala ya jinsia,VVU na UKIMWI,watoto wanaoishi katika mazingira magumu na uimarishaji wa shirika hilo.

Uzinduzi huo umefanyika leo Jumapili Desemba 22,2019 wakati wa Mkutano Mkuu wa mwaka wa shirika la Rafiki SDO uliofanyika katika ukumbi wa Karena hotel Mjini Shinyanga na kukutanisha pamoja wafanyakazi wa shirika na wadau mbalimbali.

Akizindua Mpango Mkakati wa Rafiki SDO 2020/2024, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume akimwakilisha Katibu Tawala mkoa wa Shinyanga Albert Msovela alilipongeza shirika hilo kwa jitihada ambazo limekuwa likizifanya kuwasaidia wananchi.

“Serikali ya mkoa wa Shinyanga haina mashaka na utendaji kazi wenu. Mnafanya kazi nzuri, vipaumbele vyenu ni vipaumbele vya serikali,tunawapongeza na tutaendelea kushirikiana nanyi ili kuhakikisha kuwa Mpango Mkakati huu mpya unatekelezeka kwa kiwango kinachotakiwa”,alisema Dkt. Mfaume.

“Miradi yenu imekuwa ikigusa Mipango Mikakati ya kitaifa hususani katika masuala ya elimu,afya,VVU na UKIMWI,maji na usafi wa mazingira,masuala ya ukatili wa kijinsia na uwezeshaji wanawake kiuchumi pamoja kusaidia watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi mfano watoto waliopewa ajira migodini”,alieleza Dkt. Mfaume.

Mbali na kuishukuru Rafiki SDO kwa kuwawezesha kiuchumi na kuwaondoa katika biashara ya ngono baadhi ya wasichana,aliomba shirika hilo na wadau wengine kuongeza jitihada zaidi kuwafikia baadhi ya wanawake wanaojihusisha na biashara ya ngono kwani inadhalilisha utu na kuchangia maambukizi ya VVU na magonjwa mengine ya ngono.

"Rafiki SDO mmekuwa wadau muhimu katika kuyafikia makundi maalumu ikiwemo wanawake na wasichana wanaojihusisha na biashara ya kuuza miili,mmekuwa mkiwafuata na kuwawezesha kiuchumi ili waachane na biashara hiyo. Naomba katika mpango mkakati wenu ujao muongeze jitihada kuwafikia watu hawa pamoja na watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi",alisema Dkt. Mfaume.

Aidha aliwataka wadau wote kuunganisha nguvu pamoja kupaza sauti kukabiliana na changamoto ya mimba na ndoa za utoto,malaria na UKIMWI.

Naye Mkurugenzi wa Rafiki SDO Gelard Ng’ong’a alisema Mpango Mkakati wao wa mwaka 2020/2020 umezingatia mipango mikakati ya serikali ya Tanzania hivyo wanatarajia kuwa mpango mkakati huo utaleta matokeo chanya katika mikoa wanakofanyika kazi ikiwemo Shinyanga,Mara na Simiyu.

“Mpango mkakati huu mpya umesheheni mambo mengi mazuri na yenye tija kwa wananchi kwani tumejikita kwenye maeneo muhimu ikiwemo elimu,afya,HIV/AIDs,maji na usafi wa mazingira,Jinsia wanawake na watoto, makundi maalumu na uboreshaji maisha”,alieleza Ng’ong’a.

Ng’ong’a alitumia fursa hiyo kuishukuru serikali kwa ushirikiano ambao imekuwa ikiwapatia katika kufanikisha miradi mbalimbali na kuomba ushirikiano huo uendelee kuwepo ili kuwaletea maendeleo wananchi.

“Katika Mpango Mkakati uliomalizika 2015/2019 wenye lengo la Kuwa na jamii ambayo watoto,vijana na makundi maalumu yanawezeshwa na kutambua haki zao ,Serikali na wadau mbalimbali mmekuwa nasi bega kwa bega,naomba ushirikiano huu uendelee maradufu ili kufanikisha Mpango Mkakati wa mwaka 2020/2024”,alisema Ng’ong’a.

Mkurugenzi huyo aliwapongeza wafanyakazi wa shirika la Rafiki SDO kwa utendaji kazi wao mzuri ambao umelifanya shirika hilo lijulikane na kuaminika na kuwaomba kuongeza jitihada zaidi kufanikisha utekelezaji wa miradi ya shirika.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2Zg71AY
via

Post a Comment

0 Comments