Na Leandra Gabriel, Michuzi TV
WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwele (Mbunge) amemtaka Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari nchini Mhandisi Deusdedit Kakoko kusimamia kwa ukaribu mfumo wa ukusanyaji wa mapato unaofanywa Mamlaka hiyo kwa kuwa hela inayopatikana ni kubwa tofauti na inayoashikwa na kupelekwa kwa Serikali.
Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa bodi ya wakurugenzi wa Mamlaka ya usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Waziri Kamwele amesema kuwa;
"Makusanyo yaliyo kwenye mfumo ni tofauti na hard copy (yaliyoandikwa), hela inayopatikana ni kubwa tofauti na inayoshikwa na kupelekwa serikalini, Mkurugenzi TPA lifanyie kazi suala hilo" ameeleza Waziri Kamwelwe.
Amesema kuwa bodi hiyo ya wakurugenzi lazima ihakikishe Mamlaka hiyo inafikia malengo waliyoweka na kuwataka zaidi kusimamia ukusanyaji wa mapato kwa njia za mfumo wa kieletroniki na hiyo ni sambamba na mapato hayo kuendana na yanayoandikwa na kuwasilishwa;
" Tujipongeze kwa kuwa Mamlaka hii imeongoza kwa kutoa gawio kwa serikali mwaka huu, tumetoa shilingi bilioni 480, tujitahidi katika ukusanyaji wa mapato na kutoa gawio la shilingi trilioni moja kwa serikali mwaka ujao, mapato yanavuja simamieni na kuendeleza mifumo ya TEHAMA ili ufanye kazi vizuri na kuondoa kila namna ya uvujishaji wa mapato hayo" Amesema.
Aidha amesema kuwa katika kutekeleza sera ya Serikali ya kujenga uchumi wa viwanda ifikapo 2025 hawana budi kutekeleza miradi ya kimkakati ikiwemo uboreshaji wa bandari ya Dar es Salaam unaendelea ili ukamilike kama ilivyopangwa na hiyo ni pamoja na kununua mitambo mikubwa sambamba na kuimarisha ulinzi na usalama hasa katika bandari za mipakani.
Vilevile ameitaka bodi hiyo kuendelea na kampeni za kimasoko ili kuhimili ushindani na kuongeza wateja wenye mizigo na meli.
"Tulikuta na wachimbaji wa madini na wamiliki wa meli duniani, meli ni nyingi sasa katika bandari yetu; bodi iweke mkakati maalumu wa meli kupakua mizigo kwa muda muafaka bila kupoteza Mapato" amesema.
Waziri Kamwele pia ameitaka bodi hiyo pia kusimamia ujenzi wa bandari zote katika Maziwa makuu na bahari ya Hindi pamoja na upanuzi wa bandari na kukarabati bandari nyingine za mwambao wa bahari hususani Tanga na Mtwara.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Mhandisi. Deusdedit Kakoko amesema kuwa Mamlaka hiyo itaendelea kuhakikisha ujenzi na uboreshaji wa miundombinu katika bandari zote unasimamiwa ipasavyo na hiyo ni pamoja na kusimamia ulinzi na usalama hasa katika bandari za mipakani.
Mhandisi Kakoko ameeleza kuwa utafutaji wa masoko ni jambo la msingi lenye kuhitaji ushindani na hiyo ni pamoja na kutumia mifumo ya TEHAMA; sambamba na kuboresha bandari bubu ambazo zipo 437 kote nchini ambapo bandari zenye faida zitarasimishwa ili wananchi waende sehemu sahihi zaidi na kudhibiti matumizi mabaya ya bandari hizo.
Vilevile Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi TPA Profesa. Iggnas Rabaratuka ameishukuru Serikali ya awamu ya tano kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa ushirikiano wa kujenga taifa na kusema kuwa maagizo waliyopewa yatakuwa dira katika utekelezaji wao.
Amesema kuwa suala la utekelezaji wa matumizi ya mfumo wa TEHAMA katika ukusanyaji wa mapato utachukua mwaka mmoja pekee ili mapato yafanyike katika mfumo huo hali itakayopelekea kuongezeka kwa kasi ya ukusanyaji wa mapato.
from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2ZfBbEH
via
0 Comments