Ticker

10/recent/ticker-posts

WAKALA WA BENKI YA NMB WAPIGWA MSASA

Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara Ndogo na za Kati wa benki ya NMB – Filbert Mponzi akimkabidhi msimamizi wa Rede’s Investment Traders – mmoja wa mawakala cheti cha ushiriki mafunzo ya uwakala.
Mmoja wa mawakala akiuliza swali kwa watoa mada
Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Dar es Salaam – Badru Idd akimkabidhi Agatha Makungu – mmoja wa mawakala cheti cha ushiriki mafunzo ya uwakala.
Kaimu Mkuu Kitengo cha Mawakala – James Manyama akitoa mada 

**********************************

MAWAKALA wa Benki ya NMB Halimashauri za Ubungo na Kinondoni jijini Dar es Salaam wamepigwa msasa katika Semina ya kuwajengea uwezo na kuboresha huduma inayomfikia mteja wa NMB katika maeneo yao pamoja na kujilinda na uhalifu na utakatishaji fedha.

Katika semina iliendeshwa hivi karibuni katika maeneo ya Sinza na Ilala jijini Dar es Salaam,Mawakala wa Benki ya NMB walipata fursa ya kupewa elimu juu ya kumpatia mteja huduma bora, kuuliza maswali na elimu juu ya kujikinga na vitendo vya kihalifu ikiwemo kupitisha fedha chafu, ambapo ni kinyume na sheria za nchi.

Akizungumza katika Semina hiyo Meneja wa NMB Kanda ya Dar es Salaam – Badru Idd, alisema NMB Wakala ni njia inayomfikishia huduma mteja kwa urahisi zaidi na kwa wakati.

“Kwa nini tunawatumia mawakala, tumeona kwamba ni njia moja wapo inayoweza kutufanya tuwafikie wateja wetu ambao ni watanzania zaidi ya Milioni 60, hatuwezi kufika kila eneo huwa kidogo kuna ugumu wake lakini kupitia mawakala tunaweza kuwapata kila eneo wenye uwezo wa kuwahudumia wateja wetu kama vile ambavyo tumekusudia.

“Mteja wetu anaweza kutoa pesa, kuweka pesa, ataweza kulipia miamala mbali mbali, kama kulipia malipo ya maji, umeme, malipo ya serikali na ada za shule, tunasisitiza kwamba wateja wetu waendelee kutuamini kupitia mawakala wetu ambao wanaendelea kutoa huduma.

“Tumekuwa na semina mbali mbali, tukiwa tunaendelea kuwajengea uwezo mawakala ili waendelee kutoa huduma zetu kwa ukaribu Zaidi. Muhimu ni muongozo wetu kila mwaka tunataka tuwasikilize changamoto juu ya huduma zetu, tuwaulize maswali watuulize maswali wote kwa pamoja tuweze kuhakikisha huyu mtanzania anapata huduma zetu kokote kule anakopatikana kwa ufanisi mkubwa.

Badru alisema, sio kwa Dar es Salaam tu, bali wameendesha semina kama kwa zaidi ya maeneo 40 nchi nzima. Semina hizi zimeleta mafanikio makubwa sana, hasa kwa kuokoa muda wa mteja, kupata huduma ya uhakika na kwa urahisi.

“Sisi kwetu wateja ni wafalme na ndio maana tunaendelea kuwa na huduma za mbadala kama, wakala, masine za ATM, na NMB Mkononi ili kuweza kumfikia mteja wetu kiurahisi zaidi.”alisema Badru.

Naye Kaimu Mkuu Kitengo cha Mawakala – James Manyama, alisema lengo la kukutana na Mawakala ni kuwapa muelekeo wa wapi Benki inaelekea kwa wakati na kuwapa mafunzo jinsi ya kujilinda na utakatishaji fedha pamoja na kuingiza fedha katika mikono ya gaidi.

“Kama Mawakala, tunawapa wajibu wa kutunza amana za wateja, kutunza usiri wa wateja, mawakala wetu wamethibitisha ubora wa huduma zetu na wameahidi kwenda kutoa huduma bora kwa wateja wetu” alisema Manyama.

Kwa upande wa Mawakala waliohudhuria semina hiyo walitoa kongole zao kwa NMB kwa jinsi ambavyo inawajali kwa kuwapaa elimu na fursa ya kutoa changamoto zao ili kuweza kuboresha huduma zao.

“Nafurahi sana kuwa karibu na NMB, nafurahia kuwepo katika hii semina, NMB wanatoa huduma nzuri, pia wako karibu na sisi mawakala wao, kila wakala anafanya kazi kwa ukaribu sana na tawi lake la NMB linalomhudumia, nashauri Watanzania wenzagu kuchangamkia fursa ya Uwakala wa NMB maana inalipa” Tedy Michael – Wakala NMB Makumbusho.

“Tunashukuru kwa semina hii ambayo imetupa elimu juu ya nini cha kufanya kwa wateja wetu, tumepata mbinu mbadala ya kutoa huduma bora kwa wananchi na tunawaahidi benki yetu pendwa ya NMB kuwa tutafanya kazi kwa weledi na kuhakisha wateja wanafurahia huduma zetu.” Alisema Khanifa Kimaro – Wakala NMB Kimara.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2OfHy76
via

Post a Comment

0 Comments