Ticker

10/recent/ticker-posts

TAIFA STARS YAPOTEZA MCHEZO WAKE DHIDI YA LIBYA UGENINI


Na Bakari Madjeshi, Michuzi TV

Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) imepoteza mchezo wake wa pili wa Kundi J dhidi ya Timu ya Taifa ya Libya kwa kipigo cha bao 2-1 katika mchezo uliopigwa kwenye dimba la Mustapha Ben Jannet nchini Tunisia.

Katika mchezo huo wakuwania kufuzu Michuano ya Mataifa barani Afrika yatakayofanyika mwakani nchini Cameroon, Stars ilianza kupata bao lake kupitia kwa Nahodha, Mbwana Samatta kwa mkwaju wa Penalti baada ya Mshambuliaji, Saimon Msuva kuangushwa ndani ya eneo la hatari.

Bao hilo lilidumu hadi kipindi cha Pili, Libya wakionyesha kukata tamaa na matokeo baada ya kipindi cha pili kuanza, hata hivyo dakika ya 68 wenyeji wa mchezo huo, Libya walisawazisha bao hilo kwa mkwaju wa Penalti kupitia kwa Sand Masoud baada ya Mwamuzi wa mchezo huo kudai Beki wa Stars, Bakari Mwamnyeto aliunawa mpira katika harakati za kuokoa mpira langoni.

Libya wakiwa nyumbani nchini Tunisia walionekana kupata hamasa katika dimba hilo wakianikizwa na mashabiki lukuki walifika uwanjani hapo, walipata bao la pili dakika za lala salama, dakika ya 81 kupitia kwa Mshambuliaji machachari, Anias Saltou baada ya gongana gongana ya hapa na pale katika lango la Stars.

Kwa matokeo hayo, Stars bado inabaki katika nafasi ya pili kwenye Kundi hilo J kwa alama zake 3, Kundi likiongozwa na Tunisia wenye alama 6 kibindoni baada ya ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Guinea ya Ikweta katika mchezo uliopigwa nchini Guinea.

Katika michezo ya kwanza, Taifa Stars iliifunga Guinea ya Ikweta bao 2-1 katika dimba la Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam wakati Tunisia wakipata ushindi wa bao 4-1 dhidi ya wageni Libya nchini Tunisia.



from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2qtNuQG
via

Post a Comment

0 Comments