Ticker

10/recent/ticker-posts

SHIRIKA LA KUHIFADHI MISITU ASILI TANZANIA(TFCG) LAWAJENGEA UWEZO WAANDISHI WA HABARI 28 WA KUANDIKA HABARI ZINAZOHUSU UHIFADHI


Na Said Mwishehe,Michuzi Globu-Morogoro

SHIRIKA la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania(TFCG) limeamua kuandaa mafunzo maalumu kwa waandishi wa habari nchini wapatao 28 kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kuandika habari zinazohusu usimamizi shirikishi wa wa misitu nchini.

Mbali ya kutoa mafunzo hayo shirika hilo limetumia nafasi hiyo kueleza hatua mbalimbali wanazofanya katika kuhakiksha jamii ya Watazania inakuwa na uelewa mzuri wa utunzaji misitu ya asili pamoja na kuongeza thamani ya misitu hiyo kwa jamii inayowazunguka.

Mafunzo hayo yametolewa leo mkoani Morogoro chini ya chini ya Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG), Mtandao wa Jamii wa Usimamizi Misitu Tanzania (Mjumita), Shirika la Kuendeleza Nishati Asili Tanzania (TaTEDO) ambayo yanatekeleza Mradi wa Kuleta Mageuzi Sekta ya Mkaa Tanzania (TTCS), chini ya ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Uswis (SDC).

Katika mafunzo hayo kwa waandishi wa habari, Mkurugenzi Msaidizi wa TFCG, Emmanuel Lyimo amefafanua mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo waandishi hao wa habari kuhusu rasilimali misitu inavyoweza kutunzwa na kutumika kwa faida ya jamii husika.

"Tunafahamu waandishi wa habari in kiungo muhimu kati ya jamii na watunga sera hivyo wao wanaamini kundi hilo likipata uelewa litarahisisha jamii nzima kuelewa lengo lao.Tumekuwa na utekelezaji wa mradi wa TTCS kwa takribani miaka saba sasa, hivyo wakati tunatekeleza mradi kwa wananchi waandishi wa habari ndio kiungo sahihi ya kufikisha ujumbe kwa jamii bila kupindapinda.

Hivyo tumekutana hapa kujengeana uwezo kwa kutambua waandishi wa habari ni wadau muhimu, wanafahamu mambo yanayohusu utunzaji wa misitu ya asili lakini tunataka kuelezana kwa kina kuhusu uhifadhi huo na hatimaye tuwe na lugha na tafsiri moja kati yetu sisi na wadau hasa vyombo vya habari na hii itasaidia jamii kupata ujumbe sahihi," amesema.

Amefafanua zaidi waliamua kuja na mradi huo ili kuhakikisha misitu ya vijiji inakuwa salama na endelevu jambo ambalo limeweza kuonekana kivitendo na katika maeneo ambayo mradi huo upo wamefanikiwa kiuchumi kutokana na ukweli kwamba mbali ya kutunza misitu hiyo wamekuwa wakinufaika nayo kwa kupata fedha nyingi kutokana na shughuli za uvunaji misitu unaofanywa na wanakijiji kwa utaratibu uliowekwa.

Ametumia nafasi hiyo kuelezea mradi wa mkaa endelevu ambao unasimamiwa na shirika hilo na kwamba kupitia mkaa huo endelevu umeweza kuleta mageuzi makubwa mageuzi ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wengi vijijini.Hivyo ni vema hicho ambacho wanakifanya jamii ikaelewa vema na wenye kufikisha ujumbe huo ni waandishi wa habari.

Hata hivyo amesema  misitu ni rasilimali inayoweza kukabiliana na changamoto zilizopo kwa jamii, hivyo wamekuwa wakijengea uelewa kwa wanavijiji kuhusu faida za matumizi endelevu ya rasilimali hiyo.

Kuhusu utafiti ambao umefanywa na shirika hilo, Lyimo amesema kwamba matokeo ya jumla yameonesha kuwa shughuli za kilimo ndizo zinachangia kwa kiasi kikubwa uharibifu wa misitu ya asili na hiyo inatokana na uandaaji wa mashamba mapya makubwa kwa ajili ya kilimo na hasa cha mahindi.

"Tumetembelea wilaya 67 na mikoa 22 matokeo yanaonesha ukataji wa misitu unasababishwa na uandaaji wa mashamba mapya na mkaa ni sehemu ndogo hali ambayo inachangia upotevu wa hekta 469, 000 kila mwaka,"amesema Lyimo.

Ameshauri kuwa ili kukabiliana na uharibifu wa mazingira na hasa ukataji wa misitu ni vema wanavijiji wakapewa fursa ya kuanzisha au kutenga maeneo ya uhifadhi wa misitu kwani wamebaini katika maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya hifadhi, misitu imekuwa salama kuliko ile misitu ambayo haina wa kuiangalia ambayo ndio inaharibiwa kwa kiwango kikubwa.

Kwa upande wake Ofisa wa Kujengea uwezo wa TFCG, Simon Lugazo ameongeza kuwa mradi huo umechochea kwa kiasi kikubwa jamii kutambua umuhimu wa kutunza misitu ya asili na kupata faida ya kiuchumi.Amesema hadi sasa vijiji,halmashauri na wanavijiii wamefanikiwa kuingiza zaidi ya Sh.bilioni tatu ambazo zimefanikiwa kutekeleza miradi ya maendeleo. "Fedha hizo ambazo zimepatikana kupitia mradi huo zimetumika katika miradi ya afya, elimu, kilimo, maji na uhifadhi wa misitu ukiimarika".

Wakati huo huo Ofisa Mawasiliano wa TFCG, Bettie Luwuge ametumia nafasi hiyo kutoa rai kwa waandishi wa habari kujikita katika kuandika habari zinazohusu uhifadhi wa misitu ya asili nchini.Ukweli kupitia miradi ambayo tunaisimamia kuna mafanikio makubwa katika vijiji ambavyo tunashirikiana na wananchi katika hili, tumefanikiwa sana."


Kwa upande wake Mwandishi wa Habari Mkongwe, Allan Lawa amewataka waandishi wa habari nchini kuwa wabunifu kwa kuandika habari ambazo zinagusa jamii na nchi kwa ujumla zikiwemo habari za uhifadhi wa mazingira."Iwapo waandishi wa habari watatumia kalamu zao kwa ufasaha watakuwa na mchango mkubwa kwenye sekta hiyo muhimu kwa maendeleo ya jamii".
Ofisa Mawasiliano wa Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG) Bettie Luwuge akizungumza leo kuhusu sababu za kuamua kuandaa mafunzo hayo kwa ajili ya waandishi wa habari nchini.

 Ofisa Mawasiliano wa Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG) Bettie Luwuge (wa kwanza kulia) akiwa na maofisa wengine wa shirika hilo pamoja na washiriki wengine wakifuatilia mada wakati wa mafunzo maalum kwa waandishi wa habari kwa ajili ya kujengewa uwezo wa kuandika habari zinazohusu usiamizi shirikishi wa misitu.
 Mkurugenzi Msaidizi wa Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania(TFCG) Emmanuel Lyimo akifafanua jambo wakati wa mafunzo maalumu kwa waandishi wa habari 28 kutoka vyombo mbalimbali yenye lengo la kuwajengea uwezo wa kuandika habari za uhifadhi wa mazingira na hasa misitu ya asili.
 Baadhi ya wahariri wakongwe nchini ambao wamebobea katika masuala mbalimbali yakiwemo ya uandishi wa habari za mazingira wakiwa katika mafunzo hayo.Wahariri hao ni sehemu ya watoa mada kuhusu waandishi wa habari wanavyoweza kujikita kuandika habari za mazingira na kuleta mabadiliko ndani ya jamii kujenga utamaduni wa kutunza na kuhifadhi misitu na uhifadhi wa mazingira kwa ujumla
 Ofisa wa Kujengea uwezo wa TFCG Simon Lugazo akitoa mada kwa waandishi wa habari inayohusu umuhimu wa vyombo vya habari kujikita katika kuandika habari za uhifadhi wa misitu ya asili nchini.
 Baadhi ya waandishi wa habari wakifuatilia mada zinazotolewa na wataalam wa masuala ya uhifadhi wa misitu ya asili wakati wa mafunzo hayo.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/36SFyc2
via

Post a Comment

0 Comments