Ticker

10/recent/ticker-posts

MAAJABU YA NISHATI JADIDIFU KUBAINIKA DAR


Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Maonesho hayo, Mhandisi Prosper Magali.

*Vyuo kampuni lukuki ‘mguu sawa’ kwa maonesho
ZAIDI ya kampuni 20 za nishati jadidifu, taasisi za serikali na zisizo za kiserikali, wabunifu na vyuo mbalimbali zitashiriki maonesho ya Siku ya Kitaifa ya Nishati Jadidifu Tanzania yanayoanza Ijumaa hii jijini Dar es Salaam.

Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wadau wa Nishati Jadidifu Tanzania (TAREA) ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Maonesho hayo, Mhandisi Prosper Magali, amesema maonesho hayo yatahusisha elimu, teknolojia, vifaa na huduma za nishati itokanayo na jua (solar power), upepo, na biomass.

Mhandisi Magali amezitaja baadhi ya kampuni na taasisi zilizothibitisha kushiriki maonesho hayo kuwa ni pamoja na Tirdo, Brac, Solar Sister, Ewura, Ubalozi wa Uholanzi, Carmatec,  Baraka Solar Specialist, Davis & Shirtlif, Chloride Solar, Energy Plus, Wraptec, Snv, Tarea na Ensol Tanzania Limited.

Maonesho hayo yenye kauli mbiu: “NISHATI JADIDIFU KUFIKIA TANZANIA YA VIWANDA 2025,” yatafunguliwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), George Simbachawene Ijumaa Novemba 29, 2019 na kufungwa siku inayofauata (Jumamosi Novemba 30 mwaka huu) na Waziri wa Nishati, Dk Kalemani atakayemwakilisha Waziri Mkuu.

“Kimsingi, maonesho hayo yatakayofanyika Ijumaa Novemba 29 na Jumamosi Novemba 30, mwaka huu katika Viwanja ya Mnazimmoja hapa Dar es Salaam,” alisema.

Akaongeza: “Wadau na watu mbalimbali wajitokeze kwa wingi kushuhudia teknolojia ya renewable energy (nishati jadidifu) kwa kuwa licha ya mambo mengi mazuri yatakayofanyika na kuoneshwa, hakuna kiingilio”.

Mintarafu lengo la maonesho hayo, Magali amesema ni kuionesha jamii namna Nishati Jadidifu inavyoweza kuchangia maendeleo ya Tanzania kuelekea uchumi wa viwanda ifikapo Mwaka 2025.

Ofisa wa Menejimenti ya Rasilimali wa TAREA, Cecilia Richard amesema jijini Dar es Salaam kuwa, katika maonesho hayo wataalamu mbalimbali na wadau wa nishati jadidifu watatoa elimu kuhusu mambo mbalimbali yahusuyo nishati hiyo.

“Ni nafasi pia watu waje wajue hata namna ya kubaini huduma au bidhaa feki za nishati jadidifu ili wasiangukie mikononi mwa wafanyabiashara wasio waaminifu,” alisema Cecilia.
Akaongeza: “… Tunataka tutoke kwenye zama za nishati kama za umeme kutumika kuwashia taa na kupikia pekee, sasa twende katika zama za kutumia umeme nyumbani kwa uzalishaji wa kuongeza kipato”.

Uchunguzi umebaini kuwa, maonesho hayo yanayoandaliwa na TAREA kwa ufadhili wa taasisi za Ubalozi wa Uholanzi, Energy Plus, Brac, Chloride Solar, Solar Sister na Ewura hufanyika kila mwaka.
 TAREA ni jumuiya yenye wanachama zaidi ya 796.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2XY38jt
via

Post a Comment

0 Comments