UMBALI mrefu na tatizo la usafiri ni mojawapo ya mambo yanayoelezwa kuchangia kuendeleza ukatili wa kingono kwa wanawake na wanafunzi nchini.
Hali hiyo inatajwa kuwa mbinu rahisi kwa madereva wa bodaboda na magari wakiwamo utingo kutumia kama mtego wa kuwanasa watoto wa shule za msingi na sekondari ambao husafiri umbali mrefu kuisaka elimu.
Akizungumza katika mafunzo yaliyoandaliwa na Asasi ya Wanawake Katika Jitihada za Maendeleo (WAJIKI) kwa ufadhili wa Women Fund Tanzania ya kuwajengea uwezo madereva na kuwa mabalozi katika kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia nchini ambayo imeanza Novemba 25 hadi Desemba 10 mwaka huu, Katibu wa Umoja wa Madereva wa Daladala Mbagala (UMDM), Albert Shoo anasema wanawake na wanafunzi wamekuwa waathirika wakubwa kutokana na shida ya usafiri katika mkoa wa Dar es Salaam
“ Mimi naendesha daladala ruti za Mbagala Kawe, nashuhudia mengi kwa madereva na makondakta wana msemo wa ‘Kanyagia ganda la ndizi’ hiyo ni mida ya saa tatu, nne, unawakuta bado wanasota kituoni unampakia awezi kukataa, unamsomesha unaenda kupiga mzigo (ngono) kiulaini sana,” anasema Shoo
Kauli ya Shoo imekuja ikiwa serikali tayari imetangaza kuandaa mpango wa taifa wa kutokomeza ukatili wa kijnsia dhidi ya Wanawake na Watoto kwa asilimia 50 ifikapo mwaka 2022.
Mpango huo ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia (2000); Mkakati wa Taifa wa Maendeleo ya Jinsia (2005); Sera ya Maendeleo ya Mtoto (2008); Sheria ya Makosa ya Kujamiiana – SOSPA (1998).
Kwa upande wake Mkuu wa dawati la elimu kwa umma kutoka Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru),Esther Mkokota akizungumza katika mafunzo hayo anasema madereva ni wadau wakubwa hivyo wanawajibu wa kuwalinda wanawake na watoto, wavunje ukimya na kutoa taarifa na kukemea vitendo vya ngono.
Naye Mkurugenzi wa Asasi ya WAJIKI, Janeth Mawinza anasema mbali na kudadavua mambo mbalimbali yanayochangia muendelezo wa ukatili wa kingono nchini, suala la umbali mrefu kuelekea katika shule mbalimbali nchini limechangia kuendelea kuwapo kwa ushawishi wa kushiriki ngono kwa baadhi ya wasichana na mwishowe kupata mimba.
from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2R3v8AH
via
0 Comments