Ticker

10/recent/ticker-posts

DIWANI ALALAMIKIA TEMBO KUVAMIA MAKAZI YA WANANCHI

NA YEREMIAS NGERANGERA,NAMTUMBO.

Diwani wa kata ya Mgombasi Wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma,Mrisho Mbawala aamelalamikia tembo kuvamia makazi ya wananchi wa kitongoji cha Masimango katika kijiji cha Nambecha.

Akizaungumza katika vikao mbalimbali Wilayani hapa pamoja na mkutano wa baraza la madiwani la hivi karibuni Mrisho alisema tembo katika kitongoji cha Masimango katika kijiji cha Nambecha kinawanyima wananchi uhuru wa kufanya shughuli za maendeleo ,Wanashindwa kwenda shambani wakihofia tembo .

Mrisho alidai tembo katika kitongoji hicho wametengeneza mazoea ya kuja katika kitongoji hicho mara kwa mara sio usiku tu hata mchana wanakuja na kuleta taharuki kwa wananchi alisema Mrisho.

Amedai kuwa kitendo cha kuwatumia askari wasaidizi wa vijiji (VGS) ambao hawana vifaa vya kuwafukuza tembo kinafanya tembo kuona ni jambo la kawaida kwao na kuendelea kufika katika makazi ya wananchi na kufanya uharibifu.

Mtendaji wa kata ya Mgombasi Benadetha Ndunguru alikiri kuwepo kwa tembo katika kijjiji cha Nambecha kitongoji cha Masimango ambao wanaharibu mazao ya wakulima yakiwemo mihogo,migomba na kuingia katika makazi ya wananchi .

Ndunguru alidai kikao cha maendeleo ya kata kilijadili kwa kina jambo hilo na kumtaka mheshimiwa diwani wa kata hiyo kuliwasilisha swala hilo katika vikao vya kisheria vya Halmashauri ambapo naye alifanya hivyo.

Obi Abeid Tindwa mkazi wa kijiji cha Nambecha alisema yeye anashindwa kwenda shambani kwake kutokana na tembo kufanya makazi katika mashamba yake na kuharibu mihogo,mbaazi,mapapai ,maembe,ndizi na kuvamia mahindi aliyoyahifadhi katika ghala .

Aidha kaimu mtendaji wa kijiji cha Nambecha Hamisi Rashidi Ulaya pamoja na mambo mengine alisema wameandika barua kwa Mkurugenzi wa Halmashauri kuomba askari walioajiriwa kufanya kazi ya kuwaondoa tembo hao kwani askari wa wanyamapori wa kijiji hicho (VGS) wanasusa kazi hiyo kwa madai kuwa hawana mshahara na kazi hiyo kwani hata wao wanakazi zao za shambani alisema kaimu Mtendaji huyo.

Afisa Ardhi na Maliasili wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo bwana Saimon Sambalu alidai kijiji cha Nambecha ni miongoni mwa vijiji vilivyopakana na Hifadhi ya wanyama ya Selou ambapo mara kwa mara tembo huvuka mipaka yao na kuingia katika maeneo ya karibu ya wananchi yaliyopo jirani na Hifadhi .

Hata hivyo bwana Sambalu alidai askari wao katika vijiji (VGS)pamoja na uhaba wa vitendea kazi wanajitahidi kufanyakazi ya kuwafukuza tembo hao mara kwa mara na kuwarudisha mbugani na kudai changamoto kubwa iliyopo ni kujua lini tembo hao watakuja tena baada ya kufukuzwa maana wakati mwingine wakifukuzwa humaliza hata mwezi mzima wasirudi na siku msiyotarajia wanatokea kijijini hali inayopelekea (VGS ) kuendelea kufanyakazi zao za kujipatia kipato kijijini wakidhania tembo hao wameacha kufika alisema Sambalu.

Ofisa wanyamapori wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo bwana Ernest Nombo alisema kitengo cha wanyamapori katika Halmashauri hiyo kinaendelea kuhakikisha watumishi wake wanafanya doria katika maeneo ya vijiji vilivyozunguka mbuga ya wanyama ya Selous kwa kushirikiana na askari wa vijiji waliopatiwa mafunzo kuhakikisha wanyama waharibifu wasilete madhara kwa wananchi na malizao.

Kikao cha baraza La madiwani katika Halmashauri ya Namtumbo kilitoa agizo katika idara inayohusika na wanyamapori kuwaondoa wanyama hao katika makazi ya wananchi na kuitaka idara hiyo kuacha kufanyakazi yake baada ya kutokea matukio..


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2O4mbpa
via

Post a Comment

0 Comments