Na Vero Ignatus,Killimanjaro.
Agizo limetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Siha Onesmo Buswelu kuwataka mafundi kufanya kazi mchana na usiku pamoja kuhamishia makazi yao kwa muda katika shule ya sekondari Songu inayojengwa ili waweze kukamilisha ujenzi wa shule hiyo hadi ifikapo Novemba 27 mwaka huu .
Buswelu ameyasema hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea ujenzi wa shule ya sekondari Songu na kushangazwa na ujenzi wa shule hiyo kusimama kwa muda licha ya halmashauri kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule hiyo ambapo ameiagiza Kamati ya ujenzi kununua vifaa vya ujenzi kwa muda ili kukamilisha ujenzi huo.
Mkuu huyo wa wilaya amesema kuwa shule hiyo inapaswa kukamilika haraka ili Mdhibiti ubora aweze kwenda kuikagua na kuipitisha tayari kwa kuanza kupokea wanafunzi januari 2020.
Ameainisha amesema kuwa serikali imedhamiria kusogeza huduma ya shule karibu ili wanafunzi waweze kunufaika na elimu bure inayotolewa na serikali ya awamu ya tano.
Isaya Mkilindi ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi amesema kuwa kwa sasa wako kwenye hatua ya ununuzi wa mbao na saruji hivyo watakahakikisha kazi hiyo inakamilika kwa muda na kwa wakati.
Kwa upande wao mafundi wanaojenga shule hiyo Onesmo Lyimo na Martin Yohana Kingu wamesema kuwa iwapo wataletewa vifaa vyote muhimu wako tayari kufanya kazi hadi muda wa ziada ili kukamilisha ujenzi huo.
0 Comments