Ticker

10/recent/ticker-posts

ALAT YAPONGEZA JUHUDI ZINAZOFANYWA NA AZAKI NCHINI, YAZITAKA KUSIMAMIA MALENGO YAO


Charles James, Michuzi TV

KATIBU Mkuu wa Jumuiya ya Serikali za Mikoa na Tawala za Mitaa (ALAT) Elirehema Kaaya amezitaka Asasi za Kiraia nchini (Azaki) kusimamia malengo ambayo wamejiwekea ili kunufaisha wananchi.

Kaaya amesema ni ukweli usiopingika kuwa Azaki hizo zimekua zikifanya kazi kubwa kwa kutoa elimu katika sekta mbalimbali katika kuwajengea wananchi uwezo wa kujitambua pamoja na kuwasaidia katika mambo ambayo yamekua yakihitaji msaada.

Amesema wao kama ALAT ambao wanafanya kazi katika maeneo ambayo wanakutana moja kwa moja na wananchi wamekua wakijionea mchango mkubwa unaofanywa na Azaki hizo kwa kuunga mkono juhudi ambazo zinafanywa na Serikali katika kuleta maendeleo nchini.

" Sisi kama ALAT ni wadau wakubwa wa Azaki hizi kwa sababu zinagusa moja kwa moja maisha ya wananchi wetu, na sisi kumbuka tunaziunganisha Halmashauri zote 185 na malengo yetu ni kutoa huduma mbalimbali kwa jamii hivyo nizitake Azaki hizi kuungana na Serikali kwa pamoja katika kuleta maendeleo.

Tumekua tukifanya kazi kwa karibu na Azaki hizi na kwa kweli zimekua zikionesha mchango mkubwa sana, na ndio maana tumeona ndani ya miaka mitatu wamechangia Bilioni 236 kwenye uchumi wa Nchi yetu, hii ni kuonesha wanashirikiana na Serikali yetu kuleta maendeleo chanya kwa manufaa ya Taifa letu," Amesema Kaaya.

Kaaya ametoa rai kwa Azaki hizo kujikita zaidi katika kuwajengea wananchi uwezo wa kujitegemea kiuchumi, kujenga miundombinu ya elimu, afya na kuwawezesha kujikomboa kimaisha kupitia miradi mbalimbali wezeshi ya kibiashara.

Amesema Serikali ya awamu ya tano imeweka sera ambayo Halmashauri zote nchini zinatenga asilimia 10 za bajeti zao kwa ajili ya makundi ya Vijana, Wanawake na Watu wenye Ulemavu hivyo amezitaka Azaki kujikita zaidi katika kuwajengea uwezo makundi hayo ili waweze kufaidika na mikopo hiyo.

" Mimi napenda kuona matokeo, Watu wetu wa kijijini anapenda kuona maji salama, huduma ya afya iliyo bora, nitoe rai kwa Azaki zetu nchini zijikite katika mambo yanayoonekana, tujikite katika mambo yanayogusa maisha ya watu wetu, tusiangalie sana matakwa ya wafadhili wetu bali mahitaji haswa ya wananchi ambao tumeamua kuwafanyia kazi," Amesema Kaaya.
 Katibu Mkuu Jumuiya ya Serikali za Mikoa na Tawala za Mitaa nchini (ALAT), Elirehema Kaaya akizungumza kwenye siku ya kwanza ya majadiliano ya maadhimisho ya Wiki ya Asasi za Kiraia (Azaki) yanayofanyika kwa siku tano jijini Dodoma.
Baadhi ya Washiriki wa Maadhimisho ya Wiki ya Asasi za Kiraia yanayofanyika jijini Dodoma wakiwa kwenye mijadala mbalimbali inayohusu haki za watu wenye ulemavu.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/33s15X6
via

Post a Comment

0 Comments