Ticker

10/recent/ticker-posts

WAZIRI JAFO AZINDUA MAFUNZO YA TEHAMA KWA WALIMU "TEKNOLOJIA HAIEPUKIKI"

Charles James, Michuzi TV

WALIMU nchini wametakiwa kutambua kuwa matumizi Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa wakati wa sasa ni muhimu na si jambo la hiyari kulifahamu.

Wito huo umetolewa jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Selemani Jafo wakati akizindua mafunzo ya TEHAMA kwa walimu kutoka Mikoa mbalimbali nchini iliyoandaliwa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF).

Waziri Jafo amesema katika wakati huu teknolojia ni suala la lazima hivyo ni vema kutengeneza vijana ambao ni wabobezi katika matumizi ya mifumo ya TEHAMA ili waweze kuajiriwa katika mamlaka za serikali za mitaa na maeneo mengine ambayo kwa sasa yanatumia mifumo hiyo hasa katika eneo la ukusanyaji wa mapato.

Jafo amefafanua kuwa, awali mifumo ya analojia ilikuwa ikichangia kwa kiasi kikubwa upotevu wa mapato katika mamlaka za serikali za mitaa, lakini kwa sasa mapato ya serikali yameongezeka mara dufu.

Amesema tangu mwaka 2016 walipoanza kutumia mifumo ya kielektroniki katika ukusanyaji wa mapato kwenye mamlaka za serikali za mitaa mianya ya wizi na upotevu wa mapato umekwisha.

“Nyinyi washiriki ambao ni walimu kutoka mikoa mbalimbali 1044 ni wawakilishi wa wengi waliobaki huko mashuleni, hivyo hakikisheni mnawwakilisha vyema na nitahitaji kuiona mitihani yenu nione kama kuna tofauti ya kabla ya mafunzo na baada,” Amesema Waziri Jafo.

Pia alitangaza kufanya ziara katika shule za sekondari na msingi nchi nzima kukagua kama mafunzo hayo yanatumika na kama shule zilizopatiwa kompyuta zinazitumia ama walimu wakuu wamezifungia kwenye mabox mana kunatabia hiyo.

Naye Mkurugenzi TAMISEMI anayeshughulikia Elimu, George Mbijima, amesema washiriki hao 1044 wametoka katika mikoa ambayo ni pamoja na Shinyanga, Tabora, Kigoma, Mwanza, Kagera, Geita Singida, Dodoma, ambapo walimu 1000 wanatoka katika shule za Sekondari na walimu 44 wanatoka katika shule za Msingi.

Naye wakilishi wa mfuko wa UCSAF , Justina Mashimba alisema, wamekuwa wakitoa mafunzo kuhusu TEHAMA pamopja na kugawa Kompyuta kwa walimu ambapo awamu hii watatoa kwa walimu 2000.

Amesema kundi la kwanza litahusu walimu 1044 na kundi la pili litahusu idadi ya walimu watakaokuwa wamebaki, na kwamba kundi la kwanza lina vituo 3 ambavyo ni DIT Jijini Dar Es Salaam, Dodoma na Mbeya.

Justina ameeleza kuwa mafunzo hayo walianza kutoa baada ya kubaini kuwa baadhi ya shule walimu na wanafunzi hawana uelewa kuhusu masula ya TEHAMA.
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Selemani Jafo akizungumza na walimu kutoka Mikoa mbalimbali ambao wameanza mafunzo ya siku tano ya TEHAMA jijini Dodoma.
Walimu kutoka Mikoa mbalimbali nchini ambao wameanza mafunzo ya TEHAMA ya siku tano yanayoandaliwa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote jijini Dodoma wakimsikiliza Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Selemani Jafo wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2MB9LEj
via

Post a Comment

0 Comments