Ticker

10/recent/ticker-posts

WASANII WAASWA KUJITAMBUA NA KUFANYA KAZI KWA BIDII,


Charles James, Michuzi TV

WASANII mkoani Dodoma wametakiwa kutambua thamani yao, kuwa na nidhamu na kufanya kazi kwa bidii ili kuweza kufanikiwa kwenye safari yao ya kisanii kuanzia ndani mpaka nje ya Nchi.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Patrobas Katambi wakati akizindua rasmi mchakato wa Tuzo za Nyambago ambazo zimekua zikitolewa kwa wasanii wa Kanda ya Kati.

Amesema Mkoa wa Dodoma una kipaji vingi sana lakini vinashindwa kuonekana Kitaifa kutokana na kukosekana kwa ushirikiano baina ya wasanii wenyewe kwa wenyewe, vyombo vya habari na wadau Kwa ujumla.

" Mkoa wa Dodoma una wasanii wazuri na wenye vipaji pengine kuwashinda hata ambao wameshatoka, muhimu ni kuongeza juhudi katika kazi, ushirikiano na nidhamu.

Wasanii wote wakubwa mnaowaona wamefanikiwa kwa sababu ya nidhamu na kujituma. Niwaombe mshirikiane wote hasa ndugu zetu wa Media tunaomba sana muwe msaada kwa vijana wetu hawa maana wakifanikiwa yanakua ni mafanikio yetu wote kama Mkoa," Amesema.

Akizungumzia Tuzo hizo DC Katambi amewapongeza waandaji wa Tuzo hizo kwa namna ambavyo wameendelea kujitoa kusapoti kazi kubwa inayofanywa na wasanii wa Kanda ya Kati kwani zimekua msaada wa kuwainua na kuwatambulisha zaidi kwenye sanaa.

Amesema kama wasanii wa Dodoma watatumia vizuri jukwaa la Tuzo za Nyambago wataonekana na kukua kisanii kwa haraka zaidi.

" Hizi tuzo ni kubwa ndugu zangu, kwa muda mrefu kumekua hakuna tuzo za Sanaa hapa nchini, nyie Nyambago mmeonesha uthubutu mkubwa. Hongereni na niwaambie Serikali yetu inathamini sana michezo na sanaa tutaendelea kuwaunga mkono.

" Leo siku ya uzinduzi mmenipa ugeni rasmi lakini nataka siku yenyewe ya Tukio mgeni rasmi aje mwingine lazima Wizara itambue hiki kitu kikubwa mnachokifanya kwenye sanaa yetu. Suala la mgeni rasmi siku ya kilele chenyewe niachieni mimi nitamleta," Amesema DC Katambi.

Aidha amewataka wasanii hao kutumia sanaa zao kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kwenye daftari la orodha ya wapiga kura waweze kujiandikisha ili wapate fursa ya kuwachagua viongozi wanaowataka ifikapo Novemba 24 mwaka huu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tuzo hizo, Anna Kimpa amemshukuru DC Katambi kwa kuendelea kuwa karibu nao toka walivyoanzisha Tuzo hizo ikiwa sasa ni mwaka wa pili na kuwaomba wadau wengine kujitokeza kuwaunga mkono.

Amesema Tuzo hizo zitafanyika Desemba 13 na zinashirikisha wasanii wa fani mbalimbali, wapiga picha, washereheshaji wa masherehe pamoja na watangazaji wa Radio lengo likiwa ni kuongeza ushindani na kukuza tasnia hizo Kanda ya Kati.
Mkuu wa Wilaya ya Dodoma akizungumza na wasanii wa Dodoma wakati wa uzinduzi wa Tuzo za Nyambago zinazotolewa kwa wasanii wa Kanda ya Kati. Kushoto kwake ni Mwenyekiti wa Tuzo hizo, Anna Kimpa.
 Mwenyekiti wa Tuzo za Nyambago zinazoshirikisha wasanii kutoka Kanda ya Kati, Anna Kimpa akizungumza wakati wa uzinduzi wa Tuzo hizo.


 Wasanii na Wadau mbalimbali waliojitokeza kwenye uzinduzi wa Tuzo za Nyambago ambazo hutolewa kwa wasanii kutoka Kanda ya Kati


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/31i8tSG
via

Post a Comment

0 Comments