Ticker

10/recent/ticker-posts

SHIRIKA LA RELI TANZANIA LAMSHUKURU RAIS DKT MAGUFULI KWA KUDUMISHA MAWAZO YA MWALIMU NYERERE

Shirika la Reli Tanzania – TRC pamoja na ‘Clouds Media Group’ (CMG) wameadhimisha miaka 20 ya kifo cha Baba wa Taifa Mwl. Julius Kambarage Nyerere kwa kufanya safari ya kihistoria kutoka Dar es Salaam kuelekea Dodoma kwa kutumia treni ya Deluxe kwa lengo la kuenzi mawazo ya Baba wa taifa ya kuhamasisha watanzania kuhamia makao makuu ya nchi jijini Dodoma kwa kutumia usafiri wa treni hivi karibuni, Oktoba 2019.

Katika safari hiyo Menejimenti ya Shirika la Reli Tanzania ikiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania Ndugu Masanja Kungu Kadogosa  iliungana na timu kutoka ‘Cloud Media Group’, timu ya Tigo Fiesta pamoja na wasanii zaidi ya 200 kuelekea Dodoma kuadhimisha miaka 20 ya Baba wa Taifa lakini pia kutoa burudani na hamasa kwa  wananchi wa mkoa wa Dodoma.

Licha ya kujionea Vivutio kibao vya nchi yetu ikiwemo maajabu ya mto Ruvu kwenye Safari ya kihistoria kati ya CMG na TRC, timu ya Tigo Fiesta 2019 imefanikiwa kujionea utendaji kazi wa wakandarasi waliopewa dhamana na Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kujenga Reli ya Kisasa – SGR kuanzia Dar e Salaam hadi Makutupora mkoani Singida ambapo wasanii walitembelea Kilosa katika eneo ambalo handaki refu zaidi nchini linajengwa.

Katika safari hii ya kuadhimisha miaka 20 ya kifo cha Baba wa Taifa Mwl. Julius K. Nyerere, TRC na  CMG walihakikisha uwepo wa Mwl. Nyerere ndani ya treni ambapo vitu kadhaa ambavyo vilipendwa na Baba wa Taifa vilienziwa ikiwemo mchezo wa Bao ambao alikuwa akiupenda, hotuba zake pamoja na vyakula pendwa vya Mwl. Nyerere navyo vilipikwa katika safari hiyo.

Aidha Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli alionekana akifurahia mchezo wa Bao na baadhi ya wafanyakazi wa CMG, naye ACP S.K Kulyamo, Kamanda wa Jeshi la Polisi Kikosi cha Reli pia ni moja kati ya watu ambao siku ya leo alikuwa kwenye safari ya treni kutoka Dar mpaka Dodoma kuhakikisha usalama wa wasafiri, kubwa ni kuweza kuandika historia kwa kumuenzi Baba wa taifa na kuweza kukumbuka kifo cha Baba wa Taifa ndani ya treni ikiwa ni miaka 20 toka atangulie mbele za haki.

Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana na Ajira Mhe. Anthony Mavunde amelipongeza Shirika la Reli Tanzania kwa mapinduzi makubwa yaliyofanyika katika kipindi kifupi pia amefurahi kuona wasanii wengi wameingia Dodoma kwa kutumia usafiri wa treni na anaamini kwamba wasanii wamefurahi, wamejifunza mengi na watakuwa mabalozi wazuri kuhusu usafiri wa reli pamoja na Mradi mkubwa wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa.

Mkurugenzi Mkuu wa TRC Ndugu Masanja Kungu Kadogosa kwa niaba ya Shirika amemshukuru Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kudumisha mawazo ya Mwalimu kwa kuhamisha serikali mjini Dodoma na kuboresha miundombinu ya reli ambayo ndio msingi mkuu wa usafirishaji nchini, pia amewashukuru Naibu Waziri Mhe. Anthony Mavunde, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mhe. Patrobas Katambi, timu ya CMG na wasanii kwa ujumla katika maadhimisho ya miaka 20 ya Baba wa Taifa na amesema kuwa ana imani kwamba safari hiyo iimesaidia kutunza historia kuhusu maisha ya Baba wa taifa. 



from MICHUZI BLOG https://ift.tt/35LZ2hX
via

Post a Comment

0 Comments