Ticker

10/recent/ticker-posts

Serikali yazindua mafunzo ya kilimo cha Mbogamboga, kugharimu Bilioni 2.5

Charles James, Michuzi TV
SERIKALI imewataka vijana nchini kutumia fursa zinazopatikana katika kilimo ili kujikwamua kiuchumi na kupunguza changamoto ya ajira ambayo inawakabili vijana wengi.

Hayo ameyasema Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof Joyce Ndalichako jijini Dodoma leo wakati akizindua mradi wa kuimarisha ujuzi  na uwezo wa kutoa mafunzo katika sekta ya kilimo cha mbogamboga na matunda uliodhaminiwa na Nchi ya Uholanzi utakaogharimu kiasi cha Sh.bilioni 2.5.

Prof Ndalichako amesema mafunzo hayo yatanufaisha vyuo vitatu ambavyo ni Chuo cha Kilimo Tengeru mkoani Arusha, Chuo cha Kilimo Uyole Mbeya na Chuo cha Kilimo Mahinya mkoani Ruvuma na baadaye vitatoa elimu ya ujuzi katika vyuo vingine vya ufundi.

Amesema hawawezi kufikia  uchumi wa viwanda kama hawana wataalamu wazuri waliobobea katika sekta ya viwanda.

"Kilimo ili kilete ufanisi ni lazima walime kisasa na kuachana na kilimo cha mazoea cha kutumia nguvu na ardhi kubwa badala ya kutumia maarifa, katika programu hii tunalenga wanachi wetu watumie maarifa zaidi na si nguvu kama ilivyo hivi sasa, tunaishukuru sana nchi ya Uholanzi kwa ufadhili na ushirikiano huo," Amesema.

Prof Ndalichako amewataka vijana kuhakikisha ujuzi wa mradi huo utakaotekelezwa kwa kipindi cha miaka miwili na nusu kwa kuanzia katika vyuo vitatu unatumika na kutekelezwa vizuri ili kuleta tija.

Waziri Ndalichako amesema Taifa la Uholanzi limefanikiwa sana katika kilimo na inaingiza pato kubwa kwa kupitia kilimo, hivyo kupitia chuo chao na ufadhili huu Tanzania watajifunza namna wenzao walichofanya na kufanikiwa.

Nae, Kaimu Katibu Mtendaji wa  Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE), Dk.Adolf Rutayunga, alisema tayari vyuo 530 vya binafsi na serikali vimesajiriwa tangu kuanzishwa kwa NACTE, na vyuo 87 vya Sayansi na teknolojia shirikishi vimesajiliwa.

"Leo pia tunapokea ufadhili mwingine wa zaidi ya Sh.bilioni 2 kwa ajili ya mafunzo katika sekta ya kilimo cha mbogamboga na matunda ambapo vyuo vitatu vitakwenda kunufaika," Amesema.

Akimuwakilisha Mwenyekiti wa Bodi ya Baraza la NACTE, John Kandoro, Winfrida Rutahinurwa, alisema, baraza limetoa kpmputa 400 katika vyuo mbalimbali vya elimu ya ufundi hapa nchini ili kuviwezesha kwenda ya mfumo wa sayansi na teknolojia.
 Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof Joyce Ndalichako (katikati) akiwa na Balozi wa Uholanzi nchini Jevoen Verheul wakionesha cheti kinachoashiria uzinduzi wa mafunzo ya kilimo cha Mbogamboga jijini Dodoma.
 Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof Joyce Ndalichako (katikati) na Balozi wa Uholanzi nchini, Jevoen Verheul wakikata utepe kuashiria uzinduzi wa mafunzo ya kilimo cha Mbogamboga jijini Dodoma.
Baadhi ya washiriki na wadau waliojitokeza Katika uzinduzi wa mafunzo ya kilimo jijini Dodoma.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2phEVYp
via

Post a Comment

0 Comments