Ticker

10/recent/ticker-posts

HALMASHAURI ZATAKIWA KUPITIA UPYA MAENEO YALIYOTENGWA KWA SHUGHULI ZA JAMII

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akiangalia picha zinazoonesha maeneo yaliyovamiwa wilaya ya Ilemela wakati wa ziara yake ya kukagua utekelezaji wa kupitia maeneo yaliyovamiwa katika wilaya za Ilemela na Nyamagana jana. Katikati aliyevaa Miwani ni Kamishna Msaidizi wa Ardhi Kanda ya Ziwa Makwasa Biswalo.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akiangalia moja ya eneo lililovamiwa wilaya ya Ilemela jana wakati wa ziara yake ya kukagua utekelezaji wa kupitia maeneo yaliyovamiwa katika wilaya za Ilemela na Nyamagana jana. Kushoto ni Kamishna Msaidizi wa Ardhi Kanda ya Ziwa Makwasa Biswalo.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akiangalia picha zinazoonesha maeneo yaliyovamiwa wilaya ya Ilemela jana wakati wa ziara yake ya kukagua utekelezaji wa kupitia maeneo yaliyovamiwa katika wilaya za Ilemela na Nyamagana jana. Katikati aliyevaa Miwani ni Kamishna Msaidizi wa Ardhi Kanda ya Ziwa Makwasa Biswalo.


Na Munir Shemweta, WANMM MWANZA

Halmashauri zote nchini zimetakiwa kupitia upya maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kijamii kama vile makaburi, maeneo ya wazi, ujenzi wa taasisi za umma na masoko ili kujiridhisha kama bado yanafaa kwa matumizi yaliyokusudiwa au yamevamiwa ili kurasimisha.

Agizo hilo limetolewa jana na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula wakati akikagua utekelezaji wa kupitia maeneo yaliyovamiwa katika wilaya za Ilemela na Nyamagana linalotekelezwa na wataalamu wa Ardhi kutoka Wizarani, Ofisi ya kanda ya Ziwa na Maafisa ardhi wa wilaya hizo.

Dkt Mabula alikemea kitendo kinachofanywa na baadhi ya halmashauri nchini kutolipa fidia katika maeneo wanayoyatwaa kunakosababisha kuzalisha migogoro isiyo ya lazima na uvamizi mpya katika maeneo hayo.

‘’Halmashauri zote nchini naziagiza kupitia upya maeneo yaliyotengwa kwa shughuli za kijamii tujue maeneo hayo yamevamiwa kwa kiasi gani, tuwafanyie urasimishaji wananchi walipe kodi ya serikali na kama eneo bado halijavamiwa basi tulilinde ili lisiendelee kutumika kwa matumizi yaliyo,kusudiwa ‘’ alisema Mabula

Aidha, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi aliwataka wataalamu wa ardhi nchini kuacha kukaa ofisini na badala yake waende kwa wananchi ili kuepuka kuitia hasara serikali kwa kutoa taarifa zisizo na uhakika.

Alitoa hofu wananchi wa mitaa ya Nyagungulu, Mwambani na Bukengwa yaliyopo kata ya Ilemela mkoani Mwanza kuwa, serikali ya awamu ya tano itaendelea kutatua migogoro ya ardhi kwa kuzingatia haki , sheria na ubinadamu.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Nyamagana Stanslaus Mabula, mbali na kumpongeza Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kazi kubwa anayoifanya pia alimshukuru Rais John Pombe Magufuli kwa kuunda timu ya Mawaziri kupitia maeneo yote yenye changamoto za ardhi huku akiiomba halmashauri ya jiji la Mwanza kuhakikisha ulipaji fidia kwa wananchi wenye migogoro ya ardhi unafanyika.

Naye Kmaishna Msaidizi wa Ardhi kanda ya Ziwa Makwasa Biswalo alieleza kuwa, zoezi la ukaguzi maeneo yaliyotengwa kwa shughuli za kijamii lilianza septemba 30, 2019 na kumalizika Oktoba 4, 2019 kabla ya kuongezwa siku nne na Naibu Waziri Dkt Mabula ambapo aliomba ushirikiano kutoka kwa wananchi na viongozi ili kukamilisha zoezi hilo kwa haraka na ufanisi.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/321qBS5
via

Post a Comment

0 Comments