Ticker

10/recent/ticker-posts

CHUO KIKUU CHA UDSM KUANZA KUTOA MITIHANI YA KIMATAIFA YA UJUZI WA KISWAHILI

Charles James, Michuzi TV

KATIKA kukuza lugha adhimu ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kinatarajia kuanza kutoa Mitihani ya Kimataifa ya Ujuzi wa Lugha ya Kiswahili (MKUKi) kuanzia Januari mwakani.

Mitihani hiyo itafanyika mara sita kwa mwaka ikiendana na kipindi cha masomo ya Kiswahili kwa kila ngazi na itafanyika kwa njia za kielektroniki katika vyuo na vituo vya Kiswahili duniani ambavyo tayari kuna makubaliano maalumu kuhusu mitihani hiyo.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk.Leonard Akwilapo jijini Dodoma leo alipokua akizungumza na Wandishi wa habari.

" Lengo letu ni kuunga mkono juhudi za Serikali za kukieneza Kiswahili na kusimamia ubora wake ambapo sasa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kimechukua jukumu la kuanzisha mitihani ya Kimataifa ya Ujuzi wa Lugha ya Kiswahili sanifu ili lugha ya kimataifa ipate nguvu zaidi hutungiwa mitihani ili wanaojifunza lugha hizo waweze kutathminiwa na kupata vyeti," Amesema Dk Akwilapo.

Amesema katika lugha kuu za dunia mitihani hiyo hufanyika ikiwa na majina mbalimbali kama mitihani ya Kimataifa ya Ujuzi wa Lugha ya Kichina inajulikana kama HSK na HSKK, Kihispaniola inajulikana kama DELE, Kiingereza inajulikana kama TOEFL na ya Kiarabu inajulikana kama ALPT.

Dk Akwilapo amesema Chuo Kikuu cha CKD kinakua chuo cha kwanza duniani kutunga mitihani hii na kusimamia utahinj wake na mwisho hutoa cheti cha kimataifa kuonesha kiwango cha ujuzi wa mtahiniwa.

Ameeleza kuwa tayari kuna makubaliano baina ya walimu wa Kiswahili wa CKD na walimu wanaofundisha Kiswahili katika vyuo vya nje kuhusiana na mitihani hiyo ambayo itaanza kutolewa mwakani.

”CKD kimejiandaa kuhakikisha kuwa mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano iko madhubuti kuwezesha mitihani hii kufanyika kwa ufanisi na kwa viwango vya kimataifa. Kwani kuna wahitaji ambao watafanyia mitihani hii wakiwa katika nchi zao, sio lazima wasafiri na kuja kufanyia mitihani yao hapa Tanzania,” Amesema.

Amebainisha kuwa walengwa wa mitihani hiyo ni watu wote ambao wanajifunza Kiswahili kama lugha ya pili au lugha ngeni katika ngazi mbalimbali ikilenga kupima usanifu katika kusoma, kuandika, kuongea na kusiukichangia ambapo amesema wanaamini wanapaswa kuongeza juhudi za kukuza Kiswahili ili kumuenzi Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambaye alifanya jitihada kubwa za kueneza na kukuza lugha hiyo katika Nchi za Afrika na duniani kwa ujumla.

" Serikali ya awamu ya tano imekua mstari katika kukuza lugha yetu hii adhimu ya Kiswahili. Tumeona hata wakuu wa Nchi za SADC walikubaliana kutumia lugha yetu, sasa ni jukumu letu kuongeza juhudi ili Kiswahili kiweze kuenea sehemu mbalimbali duniani," Amesema Dk Akwilapo.

Aidha Dk Akwilapo akizungumzia mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu nchini (UMISAVUTA) yanayotarajiwa kuanza kutimua vumbi Oktoba 25 ya mwaka huu mkoani Mtwara.

" Tunatarajia uzinduzi rasmi utafanyika Oktoba 27 ambapo mgeni rasmi atakua Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe ambaye atamuakilisha Waziri Mkuu ambapo yatafanyika kwa siku Sita na kushirikisha washiriki wapatao 5,600 kutoka vyuo vya ualimu vya Serikali, " Amesema Dk Akwilapo.

Ameitaja michezo itakayoshindaniwa kuwa ni Mpira wa Pete, Miguu, Wavu, Kikapu, Riadha na mashindano ya kuchora ambapo amesema lengo ni kukuza vipaji na kuwafanya walimu wawe na weledi wa kufundishia.
 Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, DK Leonard Akwilapo akizungumza na wandishi wa habari ofisini kwake Dodoma wakati alipokua akitangaza kuhusiana na mitihani ya kimataifa ya Kiswahili ambayo itaanza kutolewa na Chuo Kikuu cha UDSM. Dk Akwilapo pia alizungumzia mashindano ya Michezo kwa Walimu Nchini yatakayoanza kutimua vumbi Oktoba 25 mwaka huu.
Mkurugenzi wa Taasisi ya Taaluma za Kiswahili, Profesa Aldin Mutembei akifafanua jambo kuhusiana na mitihani hiyo ya Kiswahili ambayo itakua ikitolewa na Chuo Kikuu cha UDSM.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2Mz2dSx
via

Post a Comment

0 Comments