Ticker

10/recent/ticker-posts

Waziri Mbarawa azindua mradi wa Maji wa Milioni 331 jijini Dodoma

Charles James, Michuzi TV

SERIKALI imesema itahakikisha inakarabati miradi yote ya maji iliyoanza kujengwa tangu mwaka 2010 kwa gharama nafuu huku ikiwatumia wahandisi wazalendo lengo likiwa ni kumaliza changamoto ya maji na hasa kuendana na sera ya kumtua mama ndoo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Maji, Prof Makame Mbarawa wakati akizindua mradi wa maji katika eneo la Ng'ong'onha jijini Dodoma ambao umegharimu kiasi cha Shilingi Milioni 331.

Waziri Mbarawa amesema Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Magufuli imelenga kujenga miradi ya maji kwa asilimia 85 vijijini, asilimia 90 kwa Wilaya na asilimia 95 kwa Majiji makubwa ifikapo mwaka 2020.

Kuhusu mradi huo wa Maji wa Ng'ong'onha, Mhe Mbarawa amelishukuru Shirika la GIZ kutoka Ujerumani pamoja na Serikali ya Nchi hiyo Kwa namna ambavyo wamepambana kusaidia kukamilika kwa mradi huo.

"Niwashukuru sana wenzetu wa Ujerumani na Shirika la GIZ, hawa wameonesha kwa vitendo maana ya ushirikiano wa Nchi zetu hizi mbili ambazo kwa kipindi kirefu tumekua marafiki.

" Ombi langu kwa wananchi ambao watanufaika na mradi huu kuutunza na kila mmoja kuwa mlinzi wa mwenzake ili tuweze kutumika kwa vizazi vingi zaidi. Pia niwaahidi ndugu zetu kutoka Ujerumani kwamba sisi kama Serikali tutausimamia vizuri na hata baada ya miaka kadhaa mkiamua kuja kuutembelea muukute upo kama ulivyo leo," amesema Waziri Mbarawa.

Ameihakikishia Serikali ya Ujerumani na Shirika la GIZ kuwa Tanzania ni Nchi ambayo huwa inatumia fedha za misaada kujenga na kukamilisha miradi ya maendeleo ambayo imekua tija kwa Watanzania.

Nae Mkurugenzi wa Masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki wa Wizara ya Maendeleo ya Uchumi ba Ushirikiano wa Serikali ya Shirikisho la Ujerumani, Bi Vera Rosendahl amesema kukamilika kwa mradi huo ni mafanikio makubwa ya uhusiano wa Tanzania na Ujerumani.

Mradi huo utasaidia zaidi ya watu 12,000 ambao hawakua na uwezo wa kupata maji safi na hivyo sasa suala la ukosefu wa maji Ng'ong'onha linaenda kuwa historia.

" Kwa kufahamu umuhimu wa maji kwa wananchi na kumtua mama ndoo sisi tulitoa kiasi cha Shilingi Milioni 350 ili kuwezesha kukamilika kwa mradi huu. Tunawashukuru sana Wizara ya Maji, Halmashauri ya Jiji la Dodoma na zaidi wananchi wa eneo hili kwa namna ambavyo wametoa ushirikiano wa kutosha katika kukamilisha mradi huu," Amesema Bi Rose.

Ameahidi kuendeleza ushirikiano kwa Serikali ya Tanzania katika kuwaletea maendeleo wananchi hasa katika miradi ambayo inayagusa maisha yao moja kwa moja.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini, Mhe Anthony Mavunde ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Maji kwa ushirikiano walioutoa kukamilisha mradi huo unaoenda kuwa mwarobaini kwa wa Maji kwa wananchi wake.
Waziri wa Maji, Prof Makame Mbarawa akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mradi wa Maji jijini Dodom uliogharimu Milioni 331 na kufadhiliwa na Shirika la GIZ kutoka Ujerumani


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/31d7BzP
via

Post a Comment

0 Comments