Ticker

10/recent/ticker-posts

DC Ndejembi afunguka walivyodhamiria kuifanya Korosho kuwa zao la kibiashara

Charles James, Michuzi TV

Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Mhe Deo Ndejembi amesema mkakati wao kama Wilaya ni kuhakikisha wanahama kutoka kufanya kilimo kwa ajili ya chakula na kuwa biashara lengo likiwa ni kuunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dk John Magufuli ya kuifanya Tanzania kuwa Nchi yenye uchumi wa kati.

Hayo ameyasema katika mkutano maalumu wa Baraza la Biashara na wadau wa kilimo cha Korosho na Mtama wilayani Kongwa ambapo kwa pamoja ndani ya wilaya hiyo walikubaliana kuifanya Korosho kuwa zao la kimkakati.

Amesema kutokana na utafiti uliofanyika unaonesha kilimo cha korosho ndani ya Mkoa wa Dodoma kinawezekana na wao kama Wilaya wamechagua kuwa viongozi na vinara wa kilimo hicho ndani ya mkoa huo na hivyo wameamua kupanda michez Milioni mbili na laki mbili ndani ya Wilaya nzima.

" Ndugu zangu hii heshima ambayo Rais Magufuli ametupa ya kuifanya Dodoma kuwa Makao Makuu ni kubwa sana, lazima tuwe wabunifu kama Wilaya ili kuweza kwenda na spidi ya Mhe Rais wetu. Hivyo hizo miche Milioni mbili za korosho tutakazopanda maana yake kila kaya italima walau ekari moja yenye miche 30 ya korosho, lengo kubwa likiwa ni kuhakikisha tunakuza zao hili na kuwa zao la kibiashara lenye tija kwa wana Kongwa na Taifa kwa ujumla, " amesema Mhe Ndejembi.

Amesema mkakati huo ni muendelezo waliouanzisha miaka miwili iliyopita walipozindua kampeni ya Ondoa Njaa Kongwa (ONJAKO) na sasa wameamua iende sambamba na kampeni hii yenye kuhakikisha Kongwa inakua ya kijani na kijani yenyewe ikitokana na kilimo cha korosho.

" Tuna kaya 74,000 kila kaya moja ikilima ekari moja tunaamini kwamba tutasogea na tutakua tunatengeneza kama mzunguko wa Sh Bilioni 6 ndani ya Wilaya yetu na hiko kiwango ni cha wananchi hapo bado wakulima wakubwa watalima zaidi ya kiwango hicho na sisi kama Halmashauri tutaanzisha ekari 1000 ili kukuza zao hili," amesema DC Ndejembi.

Amesema mkakati wa kilimo cha korosho katika Wilaya ya Kongwa ni uwezeshaji wa wananchi kiuchumi ambao ni utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/20. MKUKUTA na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 ili kufikia uchumi wa kati.


from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2ZHuqOD
via

Post a Comment

0 Comments