Ticker

10/recent/ticker-posts

Unayetembea na mume, mke wa mtu soma hapa!

LICHA ya kuwepo na msemo wa mke au mume wa mtu ni sumu bado watu wengi wameendelea kutenda tendo hilo. Hawahofii madhara yake. Wanaona kama ni jambo la kawaida. Wanahalalisha jambo hilo utafikiri kufanya hivyo ndiyo jambo jema.
Kutembea na mke au mume wa mtu ni tabia. Huanza taratibu na baadaye hukua. Kama vile ilivyo kwa mlamba asali, kadiri anavyopata utamu ndivyo anavyozidi kulamba. Kila anayefanya kitendo hiki huwa na sababu zake.
Kuna ambao wanaingia kwa sababu ya mawazo. Alikuwa na mpenzi au mchumba wake wakaachana, ghafla anajikuta ameingia katika penzi la mke au mume wa mtu kwa sababu ndiye aliyempata kwa wakati huo.

Wengine wanaingia katika janga hili kwa sababu ya tamaa tu. Wengi sana wanaingia kwa sifa hii. Wanataka maisha mazuri hivyo wakiyaona yanapatikana kwa mke au mume wa mtu, wanaingi. Hawaangilii matokeo ya baadaye, zaidi tamaa ndizo zinazomuongoza.

Hapo ndipo unapokuta mwanamke anapokubali kufanywa chombo cha starehe. Mume wa mtu anayetembea naye anamtumia kama chombo cha kumuondoa mawazo yake. Anamfanya kama chombo cha kumstarehesha pale anapokuwa amegombana na mkewe.
Bahati mbaya zaidi mwanaume wa aina hiyo hupenda kuumiliki huo mchepuko wake. Hataki amuone na mwanaume mwingine. Anahakikisha kwa kila namna anamfunga kwa kila njia anayoijua ilimradi asichepuke.
Anahakikisha anampatia kila kitu. Kama ni fedha, nyumba na hata magari ya kifahari anampa. Anafanya hivyo ili asisalitiwe. Na akithubutu kufanya hivyo lazima mhusika akione cha moto. Hapo mwanamke hana ujanja, anakubali kuepusha shari.

Matokeo yake anajikuta anapoteza muda. Anashikiliwa na mtu ambaye tayari ana mtu wake rasmi. Yeye ni wa ziada lakini mwanaume anamfunga asipate mtu mwingine. Atazalishwa, atalea watoto na kujikuta uzee ukimnyemelea pasipo kuwa na ndoa.

Vivyo kwa wanaume, nao wanapoteza muda. Wanajikuta wameshikiliwa na wanawake wenye fedha. Hawataki wawe na wanawake wengine. Wanaume hao nao pia hupoteza muda. Lakini wengine huingia kwenye tabia hii kwa tamaa za kimwili.
Kila anayekutana naye anataka awe wake. Haijalishi ni mke au mume wa mtu, yeye anamtamani na kumtaka awe wake. Marafiki zangu, kuna kila sababu kila mmoja wetu kujiuliza mara mbilimbili kabla hujaamua kuchepuka na mume au mke wa mtu.
Fikiri kuhusu madhara ya kupoteza muda. Fikiri kuhusu mustakabali wa maisha yako ya baadaye. Utatumika hadi lini? Utakuwa mtumwa wa fedha hadi lini? Tamaa zako zitakufikisha wapi? Kwa nini usimpate wako? Utakayekuwa na uhuru naye.

Mume au mke wa mtu huwezi kuwa na uhuru naye. Atatumia muda mchache kwako lakini bado atalazimika kuihudumia familia yake. Wewe utabaki kuwa wa ziada. Bahati mbaya anakubana wewe usioe au kuolewa na mtu mwingine.
Kuna umuhimu wa wewe kuwa na mchumba wako. Mtakayeanza na kumaliza pamoja safari ya hapa duniani. Mtu ambaye mtaelewana kwa kila hali, mtafikia hatua ya kufunga ndoa na kulea familia yenu pamoja.
Utakuwa mtu wa wiziwizi. Hujiamini. Utazaa au kuzalishwa watoto wa nje ya ndoa. Jambo hilo ni hatari pia katika mustakabali wa watoto. Ndoa wewe utazisikia kwa wenzako. Ni jukumu lako kuchagua njia iliyo sahihi. Kuchagua mwenza sahihi pasipo kusukumwa na jambo lolote.
Maisha ya uhusiano ni zaidi ya fedha. Uhusiano ni utu. Mtu ambaye mtajaliana kwa kila jambo. Katika shida na raha. Katika uzima na magonjwa, hayo ndiyo maisha mazuri ya uhusiano. Kinyume na hapo ni janga. Utafurahia maisha kwa kipindi fulani, baadaye utapata machungu.
Kwa leo ni hayo tu, tukutane wiki ijayo kwa mada nyingine nzuri ya kusisimua