Ticker

10/recent/ticker-posts

Sasa Viza za Israel zaanza kutolewa hapa nchini, faida zake zabainishwa

Serikali ya Israel imeanza kutoa huduma za viza moja kwa moja kutokea jijini Dar es Salaam ambapo kwa mujibu wa Waziri wa Maliasili na Utalii Profesa Jumanne Maghembe, hatua hiyo itachochea ukuaji wa biashara pamoja na ushirikiano wa kidiplomasia.

Awali, viza zilikuwa zikitolewa jijini Nairobi nchini Kenya lakini hivi sasa huduma hiyo itakuwa ikipatikana jijini Dar es Salaam ambapo Waziri Maghembe ametaja baadhi ya faida chache za utolewaji wa huduma hizo hapa nchini kuwa ni kupungua kwa urasimu na gharama za kutafuta viza, kukua kwa ushirikiano katika nyanja zote za uchumi, elimu ulinzi pamoja na usalama.

Balozi wa Israel nchini Kenya Bw. Yahel Vilan amesema hatua hiyo itakuza uhusiano wa kidiplomasia hususani kwenye eneo la uchumi, kutokana na uzoefu mkubwa iliyonao taifa hilo ambalo hivi sasa limepiga hatua kubwa kwenye uchumi na teknolojia.

Kwa upande wake, Bi. Pooja Lalji amesema wamejipanga kuhakikisha wafanyabiashara wanaokwenda Israel wanapata viza zao mapema na hivyo kuchochea biashara baina ya Tanzania na taifa hilo la Mashariki ya Kati