Ticker

10/recent/ticker-posts

Mbunge Hussein Bashe afunguka mapya kuhusu Lowassa , Aeleza Uhusiano wao Kwa Sasa


Mbunge wa Nzega, Hussein Bashe (CCM) amesema kuwa anaamini waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa aliondolewa kwa kuonewa katika mchakato wa kugombea urais ndani ya CCM.

Bashe amesema kuwa kitendo hicho alichokiita cha kiuonevu ni changamoto kubwa ndani ya CCM na kwamba wengi wameonewa katika michakato ya kuwania nafasi mbalimbali.

“Yaliyomkuta Lowassa yamewakuta wengi ndani ya CCM, hivyo jambo hilo sio geni,” Bashe anakaririwa na Mwananchi. “Wapo waliobaki na wapo walioamua kuhama chama kwa sababu ni binadamu. CCM ina historia hiyo, hii ndiyo changamoto yake kubwa,” aliongeza.

Mbunge huyo alifafanua kuwa kwakuwa Lowassa alituhumiwa kwa mengi ndani ya chama hicho, alipaswa kuitwa na kuelezwa tuhuma zake na sababu za kuondolewa jina lake ili umma ufahamu.

Alisema kuwa katika chama hicho, kashfa nyingi hufanywa kwa sababu maalum na hubuniwa kwa ajili ya kufikia lengo fulani dhidi ya mtu au kikundi cha watu.

Alisema kuwa mbali na sakata la Richmond lililopelekea Lowassa kujiuzulu nafasi ya uwaziri mkuu, masakata ya Lugumi na Tegeta Escrow ni sehemu yale yaliyobuniwa kwa lengo maalum.

“Tazama wanavyofunika sakata la Lugumi. Usiende mbali angalia sakata la Escrow. Tumeadhibu waliopata fedha kutoka benki ya Mkombozi, vipi wa Stanbic? Wizi mwingine uliofanywa nchi hii una uhusiano kati ya Serikali na vikundi vya watu wenye uhusiano na Serikali,” Bashe aliliambia Mwananchi.

Akizungumzia uhusiano wake na Lowassa ambaye alikuwa anamuunga mkono wakati wa mchakato wa kugombea urais kupitia CCM, Bashe alisema hivi sasa hawana uhusiano tena wa urafiki wa kisiasa.

Alisema kuwa alimshauri sana Lowassa kutohama CCM, avumilie, lakini hakufanikiwa kumshawishi, hivyo waliagana.

“Lowassa ni mzee wangu. Ni mtu ambaye namheshimu na nitaendelea kufanya hivyo, ingawa kwa sasa hatuna uhusiano wa kisiasa,” alisema.

Lowassa alihama CCM baada ya jina lake kukatwa katika mchakato wa kuwania urais, alihamia Chadema na kupewa nafasi ya kugombea urais katika uchaguzi unaotajwa kuwa na ushindani mkali zaidi tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi.